Kaimu Mkurugenzi, Kurugenzi ya
Usimamizi na Uendeshaji wa Mashauri kutoka Mahakama ya Tanzania, Bw. John
Kahyoza (kushoto), akiwaeleza Waandishi wa Habari (hawapo pichani), mikakati iliyowekwa na Mahakama ya Tanzania, ili kutekeleza dira yake ya haki sawa
kwa wote na kwa wakati kwa vitendo, kwa kuhakikisha inapunguza muda wa
mashauri kukaa mahakamani, wakati wa mkutano uliofanyika leo Jijini Dar
es Salaam. Kulia ni Afisa Habari wa Mahakama ya Tanzania, Bi. Mary Gwera.
Na Mwandishi wetu.
Mahakama ya Tanzania imedhamiria kutekeleza dira yake ya haki
sawa kwa wote ili kuhakikisha inapunguza muda wa mashauri na rufaa kukaa
Mahakamani kwa muda mrefu.
Hayo yamesemwa na Afisa Habari wa Mahakama ya Tanzania, Bi. Mary Gwera, wakati wa mkutano uliofanyika leo Jijini Dar es Salaam.
Akizitaja hatua zilizochukuliwa na Mahakama, Bi Mary alisema,
kuboresha bajeti ya kushughulikia mashauri kupitia mfuko wa mahakama
toka bilioni 57 kwa mwaka 2012/13 mpaka bilioni 88 mwaka 2014/15, idadi
ya vikao vya Mahakama ya Rufani vimeongezeka kutoka 26 mwaka 2012 hadi
34 mwaka 2013/14.
Aidha, Bi Mary alisema kuwa, hatua nyingine ni pamoja na
kuanzisha kitengo cha Mahakama Kuu Dar es Salaam kitakachoshughulikia
masuala ya utatuzi wa mashauri kwa njia ya suluhu muafaka, pia uundwaji
wa kamati ya kanuni za Mahakama itakayosaidia kutunga au kurekebisha
kanuni ili kuhakikisha kuwa kanuni zinazotumika Mahakamani si chanzo cha
kuchelewa mashauri Mahakamami.
Naye, Kaimu Mkurugenzi, Kurugenzi ya Usimamizi na Uendeshaji wa
Mashauri kutoka Mahakama ya Tanzania, Bw. John Kahyoza, alisema kuwa
Mahakama imeanza kuchukua hatua za kuimarisha ukaguzi wa shughuli za
Mahakama na maadili ya watumishi kwa kuanzisha kurugenzi ya ukaguzi na
maadili.
Aidha Bw Kahyoza, alivitaja viwango ambavyo kila hakimu au Jaji
anatakiwa kuvitimiza kwa mwaka na muda ambao mashauri yanatakiwa kuwa
Mahakamani kuwa ni Mh. Jaji wa Mahakama Kuu analenga kumaliza kesi 220,
Mahakimu wa Mahakama za Wilaya na Hakimu Mkazi kesi 250 na Mahakimu wa
Mahakama za mwanzo kesi 260.
Mahakama Kuu inatoa rai kwa Watanzania kufika Mahakamani kwa
Tarehe zinazopangwa ili kuisaidia Mahakama kuhakikisha inapunguza muda
wa mashauri kukaa Mahakamani.
No comments:
Post a Comment