Meneja wa Maudhui na Vipindi wa StarTimes Tanzania, Bi. Paulina Kimweri akizungumza na waandishi wa habari (hawapo pichani) wakati wa uzinduzi wa tamthiliya ya ‘Scars’ itakayoanza kuonekana siku ya Jumatatu ya Mei 2, 2016 kupitia chaneli ya StarTimes Swahili. Akimsikiliza kwa makini katika uzinduzi huo uliofanyika katika ofisi za kampuni hiyo mwishoni mwa wiki jijini Dar es Salaam, kulia ni Meneja wa Uhusiano wa Umma, Bw. Muddy Kimwery. |
Katika kuboresha maudhui
yanayotumia lugha ya Kiswahili, kampuni ya StarTimes Tanzania kupitia
chaneli yake mahususi kwa vipindi vya Kiswahili ya StarTimes Swahili
imewatangazia wateja wake ujio wa tamthiliya mpya na ya kusisimua ya
‘Scars au Makovu’ itakayoanza kurushwa siku ya Jumatatu ya mwezi Mei 2,
2016 saa 2:30 usiku.
Akizungumza na waandishi wa
habari wakati wa uzinduzi wa tamthiliya hiyo Meneja wa Vipindi na
Maudhui wa StarTimes Tanzania, Bi. Paulina Kimweri amebainisha kuwa
tamthiliya ya ‘Scars’ itakuwa ni ya aina yake na kusisimua zaidi kwani
inagusa zaidi maisha halisi ya kila siku.
“Tamthiliya hii ni tofauti na
zingine kwani ndani yake ina visa na simulizi za kweli kabisa za maisha
ya wahusika waliocheza ndani yake. Masuala kama ya changamoto mbalimbali
wanazopitia watu kwenye familia zao kama vile mateso, udhalilishaji na
unyanyasaji wanaopitia wanawake katika ndoa zao. Haya yote yatakuwa
yakisimuliwa na kuonekana kwa wateja na watazamaji wa chaneli ya
StarTimes Swahili.” Alielezea Bi. Kimweri
Meneja huyo wa Maudhui katika
kampuni hiyo inayotoa huduma ya matangazo ya luninga kwa njia ya
dijitali alifafanua zaidi kuwa, “Lengo kubwa la kuanzishwa na kuwepo kwa
chaneli hii mahususi kwa vipindi vya Kiswahili si tu kuwaburudisha
wateja wetu kwa maudhui mazuri bila pia kukuza lugha ya Kiswahili kwani
chaneli hii inaonekana katika nchi za Tanzania na Kenya. Pia hutoa fursa
kwa watayarishaji na wasanii wa vipindi vya Kiswahili baina ya nchi
hizi. Hivyo basi hii ni fursa kubwa ya kufurahia wasanii wetu na
kuipaisha lugha yetu ya Kiswahili ambayo kwa sasa inazidi kupaa katika
anga za kimataifa.”
“Nina imani kubwa na tamthiliya
hii ya ‘Scars’ kwamba itapendwa sana na wateja wetu kwani inagusa maisha
halisi kwa simulizi zitakazopatikana ndani yake. Katika uchaguzi wa
tamthiliya tunazotaka zionekane kwa wateja wetu huwa tunazingatia sana
suala la ujumbe na mafunzo yanayopatikana ndani yake na si burudani
pekee. Hivyo, basi ningependa kuchukua fursa hii kuwataka wateja wetu na
watanzania wapenda tamthiliya tamthiliya kukaa mkao wa kula na kutega
macho ya mbele ya luninga zao ifikapo siku ya Jumatatu na zinginezo kila
ifikapo saa 2:30 usiku kwenye chaneli ya StarTimes Swahili. Nawaomba
walipie kwani malipo yetu ni nafuu ili kila mtu aweze kufurahia huduma
zetu.” Alihitimisha Bi. Kimweri
Mbali na tamthiliya mpya ya
‘Scars au Makovu’ pia kupitia chaneli ya StarTimes Swahili ambayo
inaonekana kwenye kisimbuzi cha kampuni ya Startimes kwa nchi za Kenya
na Tanzania pia kuna tamthiliya moto moto zinazoonekana kwa sasa kama
vile; Urembo, Fihi, Majaribu, Kijakazi, Majaribu, Kivuli na Sumu la
Penzi.
Chaneli hii imeanzishwa mahususi
kabisa katika kuonyesha vipindi vyenye maudhui ya lugha ya Kiswahili
ambapo lugha hiyo inazungumzwa katika nchi nyingi za Afrika ya Mashariki
na Kati. Kupitia chaneli hii si tu kukuza lugha ya Kiswahili bali pia
ni fursa kubwa kwa wasanii kuonekana na kujitangaza kupitia kazi zao ili
ziweze kuonekana katika soko la Afrika ya Mashariki. Hivyo basi hii
fursa kubwa kwa wasanii wa nchini Tanzania kuchangamkia faida zinazokuja
na matangazo ya dijitali kwa kupeleka kazi zao katika kampuni ya
StarTimes ili ziweze kuonekana hewani.
|
No comments:
Post a Comment