Baada ya Kamati ya
Nidhamu ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) kumfungia mechi mbili beki
wa Simba, Abdi Banda ambapo tayari adhabu hiyo ameshaitumikia, beki huyo
amesema hatarudia tena kosa hilo.
Aprili 2, mwaka huu,
Banda aliingia matatizoni kwa kumpiga ngumi nahodha na beki wa Kagera
Sugar, George Kavila kwenye Uwanja wa Kaitaba, Bukoba wakati timu hizo
zikipambana.
Banda alipelekwa
kwenye Kamati ya Nidhamu kwa kosa hilo la kumpiga Kavila na kuadhibiwa
kwa adhabu ambayo alishaitumikia kwani alisimamishwa kucheza mechi
yoyote hadi suala lake litakaposhughulikiwa.
Akizungumza Banda
alisema: “Namshukuru Mungu suala langu limeisha, nimekoma na kuna kitu
nimejifunza maana nilijiona mkosefu kwa kujadiliwa na watu wengi.
“Sitarudia tena
kitendo kama kile licha ya mchezo wa soka kuwa na majaribu mengi ambayo
yanaweza kukufanya uchukue uamuzi wowote ule, nimejifunza na kuanzia
sasa mimi ni mtu mwema.
“Kusimamishwa mechi
mbili hakukuniathiri kwa kuwa mimi ni mchezaji mkubwa ila
ninachokiangalia hivi sasa ni kuisaidia timu yangu iweze kutwaa
ubingwa.”
Hata hivyo, kanuni za
ligi kuu zinaweka wazi kwamba mchezaji anayepigana au kupiga uwanjani
anafungiwa kucheza mechi tatu au zaidi, habari kutoka kwenye kamati hiyo
zinasema Banda aliomba msamaha.
No comments:
Post a Comment