KWA MAONI AU USHAURI E-mail: inocomm2014@gmail.com, PIGA SIMU: 0714555668

www.utt-pid.org


TEMBELEA: www.utt-pid.org

September 21, 2017

TULIA TRADITIONAL DANCE FESTIVAL YAANZA KWA MBWEMBWE NA BASHASHA


Kikundi cha  ngoma yaasiliya Sindimba toka mkoa wa Mtwara,Wakicheza ngoma hiyo jana wakati wamashindano ya ngoma za asili yaliyodhaminiwana Vodacom Tanzania PLC ya”Tulia Traditional dances festival 2017”yanayofanyika kwa siku tatu katika viwanja vya tandale mjini tukuyu wilayaya Rungwe mkoa wa Mbeya.
TAMASHA la ngoma za kitamaduni lililopewa jina la Tulia Traditional Dance Festival, limeanza kwa mbwembwe mjini Tukuyu, mkoani Mbeya jana, likishirikisha vikundi zaidi ya 100 kutoka maeneo mbalimbali hapa nchini ambapo litafikia tamati kesho.  

Akizungumza tamasha hilo akiwa Tukuyu jana, Naibu Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Tulia Ackson ambaye ndiye mwasisi wake, alisema kuwa anajisikia furaha kuona tukio hilo limepokewa vizuri mno na wakazi wa Tukuyu na mkoani Mbeya, lakini pia na Tanzania kwa ujumla.

“Maandalizi yanaendelea vizuri na mwitikio umekuwa mkubwa mno kuonyesha jinsi Watanzania wanavyothamini tamaduni zao. Matamasha kama haya ni muhimu mno kwani hutoa fursa ya kutangaza utamaduni wetu wa kitanzania na kuwa moja ya kivutio badala ya kutegemea vivutio vya kiutalii vilivyozoeleka kama Mlima Kilimanjaro, mbuga na hifadhi za wanyama na vinginevyo.

“Nawaomba wabunge waandae matamasha kama haya katika maeneo yao ili baadaye washindi watakaopatikana, waweze kushiriki katika tamasha letu hili ili kulifanya kuwa la kitaifa zaidi, hii itasaidia kuwaonyesha vijana wetu wa kizazi cha sasa kufahamu tamaduni zao, kuona mababu zao walikuwa wakifanya nini.

“Kwa serikali, iandae na kuunga mkono matamasha ya utamaduni kama sehemu ya kuenzi utamaduni wetu kwani vijana wengi wamekuwa wakibobea katika tamaduni za kigeni kutokana na kutofahamu tamaduni zao,” alisema.

Aliipongeza kampuni ya Vodacom kwa kujitosa kudhamini tamasha hilo la aina yake ambalo anaamini litafana vilivyo mwaka huu.

Alisema tamasha hilo limeshirikisha vikundi zaidi ya 100 kutoka mikoa mbalimbali, hali inayotoa picha kuwa kwa sasa ni tukio la kitaifa, akiwataka wanasiasa, hasa wabunge, mashirika, taasisi na kampuni mbalimbali kujitokeza kulidhamini.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Mawasiliano na Uhusiano wa Vodacom Tanzania, Rosalynn Mwori, alisema kuwa huu ukiwa ni mwaka wao wa kwanza kudhamini tamasha hilo, wanajisikia fahari kubwa kuungana na Muheshimiwa Dk Tulia kusapoti tukio hilo, wakiwa kama miongoni mwa wadau wa masuala ya burudani, michezo na mambo ya kijamii.

“Vodacom Tanzania tunajisikia fahamu kuwa sehemu ya tamasha hili kupitia udhamini wetu, tumeona ni vema kudhamini tamasha hili kwani lina manufaa makubwa kwa jamii ya kitanzania, hasa katika suala zima la kuuenzi utamaduni wa Mtanzania,” alisema.

Aliongeza: “Kama kila mmoja wetu anavyofahamu, Vodacom Tanzania imekuwa mstari wa mbele katika kusapoti matukio mbalimbali ya kijamii kama sehemu ya kuionyesha jamii jinsi tunavyoijali kwani ndio wadau wetu wakubwa waliotuwezeshja leo hii kuwa mtandao bora kabisa wa mawasiliano hapa nchini.”

Alisema kama ambavyo wamekuwa wakisapoti matukio mbalimbali ya kimichezo na utamaduni kama vile udhamini wao wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara, mashindano ya Dance 100%  na mengineyo, wataendelea kudhamini tamasha hilo miaka ijayo kadri itakavyowezekana.

Aliwataka wadau wengineo wa sanaa na burudani kwa ujumla hapa nchini kujiotokeza kudhamini tamasha hilo ambalo anaamini linaweza kuwa dira ya utamaduni wa Mtanzania iwapo litapewa sapoti inayostahili.

Naye mkazi wa Iromba, Mbaye ambaye amehudhuria tamasha hilo, Kenneth Sanga, alilimwagia sifa tamasha hilo akisema kuwa linakumbusha tulikotoka likitoa fursa kwa vijana wa sasa kufahamu watu wa zamani walikuwa wakifanya nini.

“Kuna watu wa kutoka maeneo mbalimbali wamehudhuria tamasha hili, hili ni jambo kubwa sana hivyo ni vema serikali ikaunga mkono jitihada hizi zilizoonyeshwa na muheshimiwa Dk Tulia kwa kuendesha matamasha kama haya katika maeneo mbalimbali nchini,” alisema Sanga.




No comments:

Post a Comment