November 29, 2016

MIAKA 55 YA UHURU: SERIKALI YAENDELEA KUPIGA HATUA KATIKA DHANA YA KUJITEGEMEA.

2NA Daud Manongi – MAELEZO
Mhadhiri Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam Profesa Haji Semboja amesema kuwa Serikali imepiga hatua kubwa kutekeleza dhana ya kujitegemea katika maendeleo ya Taifa kuelekea miaka 55 ya Uhuru wa Tanzania Bara.
Profesa Semboja amebainisha hayo leo Jijini Dar es Salaam wakati wa mahojiano maalum na mwandishi wa habari hizi kuhusiana na hatua mbalimbali ambazo Serikali ya awamu ya Tano imezifanya.
Ameeleza kuwa Serikali ya Awamu ya Tano chini ya Uongozi wa Rais John Pombe Magufuli imeweka kipaumbele katika kusimamia matumizi yake na kuongeza ukusanyaji mapato na kubadili mifumo ya kisera pamoja na kupunguza kutegemea misaada ya nje.
“Wakati wa Uhuru hayati Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere aliweka kipaumbele katika kupambana na Ujinga, Maradhi, Umaskini na Rushwa, na hilo limeendelea katika awamu zote nne na hivyo kwa nyakati tofauti Taifa limeweza kusonga mbele na na mfumo wa ujamaa na kujitegemea pia ulitufanya kutambulika vyema Duniani,” Alisema Profesa Semboja.
Aidha amesema kuwa kuanzia mwaka 1961 Serikali zetu za awamu tano zimejikita katika kuijenga Jamii pamoja na soko Huria kwa ujumla.
Kwa upande wa maboresho katika Utumishi wa Umma anasema kuwa uwajibikaji ulikuwa umedorora lakini kwa sasa umerudi katika hali nzuri kutokana na usimamizi kuwa bora na pia idadi ya watumishi imeongezeka na Ubora wa elimu umekuwa wa hali ya juu.
Aidha anaongeza kuwa hali ya kiuchumi na afya imeboreka na kuzidi kufanya maendeleo ya jamii kuwa bora zaidi.
Maadhimisho ya miaka 55 ya uhuru mwaka huu yanafanyika tarehe 09/11/2016 katika viwanja vya Uhuru jijini Dar es Salaam huku kauli mbiu ikiwa ni “Tuunge Mkono Jitihada za Kupingaji Rushwa, Ufisadi na Kuimarisha Uchumi wa Viwanda kwa Maendeleo Yetu”.

No comments:

Post a Comment