KWA MAONI AU USHAURI E-mail: inocomm2014@gmail.com, PIGA SIMU: 0714555668

www.utt-pid.org


TEMBELEA: www.utt-pid.org

March 15, 2018

RC TABORA AMWAGIZA OCD KUWATIA MBARONI WATU WAWILI

               Mkuu wa Mkoa wa Tabora Aggrey Mwanri amemwagiza Mkuu wa Polisi Wilaya (OCD) ya Kaliua kuwakamata watu wawili kwa tuhuma mbalimbali ikiwemo moja  kuchukua chupa 50 dawa za kuua wadudu katika zao la pamba na mwingne kutumia mzani wa rula uliopigwa marufuku kwa kuwa inatumika kuwanyonya wakulima.
               Mwanri alitoa agizo hilo jana katika maeneo mbalimbali Wilaya Kaliua Mwanri  wakati wa kampeni zake kuelimisha wakulima wa pamba mkoani humo juu ya upuliziaji sahihi wa dawa za kuua wadudu katika zao hilo.
                Katika tukio la kwanza lilimhusisha Wakala wa Kampuni ya Kahama Cotton Company Limited (KCCL) wa Kata za Seleli na Kona Nne Boniface Kibiru anayetuhumiwa kuchukua dawa za kuua wadudu wa pamba bila kufuata sheria na taratibu na hivyo kusababisha fujo kwa wakulima wa zao hilo kwa hofu ya wadudu kuathiri mazao yao shambani kwa sababu ya kukosa dawa hizo.
                “OCD mtafute alipo mtuhumiwa huyo …kamata na mpeleke Mahakamani kwa tuhuma za wizi kwa sababu ushahidi upo …wananchi na viongozi wa kijiji wametueleza kuwa mhutumiwa alichukua chupa 50 za dudu ba jambo ambalo lilisababisha usumbufu mkubwa kwa wakulima wengi na kuathiri mazao yao kwa sababu ya kuwachelewesha kupiga dawa za kuua wadudu wakati wakisubiri muafaka” alisema Mkuu huyo wa Mkoa.
                  Alisema chupa hizo 50 alizochukua mtuhumiwa zingeweza kunyunyuzia ekari 50 za pamba, kwa hiyo kitendo hicho ni sawa na wizi na hivyo  lazima apelekwe Mahakamani ili akaeleze hizo chupa alikuwa anazipeleka wapi.
                 Naye Mtendaji wa Kijiji(VEO)  cha Mwendakulima Regina Kataka alisema tukio hilo lilitokea baada ya kutoka kuchukua dawa hizo katika eneo la Seleli alipokuwa ametumwa kuzifuata  na ndipo baada ya kuzifikisha alichukua chupa 50 bila kufuata utaratibu na kubakiza 150.
                  Alisema kesho wakiwa wanatarajia kuanza kugawa dawa hizo kwa ajili ya kusaidia wakulima ndipo walipogundua upungufu katika makasha na wakaamua kumhoji naye akakiri kuchukua chupa hizo kwa matumizi ya mashamba yake.
                     VEO alisema kitendo hicho kilichosababisha kuchelewesha zoezi la kuanza ugawaji dawa kwa wakulima kilisababisha malalamiko na usumbufu kwa wakulima na ndipo walipoitisha kikao na kuamua kumpa adhabu ambaye baadaye aliikataa kuitekeleza.
                     Alisema kuwa Kijiji hicho kina wakulima 500 ambao wamelima ekari 920 katika eneo hilo.
                        Akiwakilisha kero yake kwa Mkuu wa Mkoa Mwanakijiji wa Mwendakulima Manane Mwalemi alimwomba Mkuu wa Mkoa wa Tabora amchukulie hatua mtuhumiwa huyo baada ya kuwasababishia usumbufu na athari kubwa katika zao lao la pamba baada ya kuwafanya wachewe kunyunyuzia dawa na hivyo wadudu kuathiri mazao yao.
                         Alisema awali katika kikao chao kijiji cha kumhoji Mtuhumiwa na yeye kukiri kutenda kosa hilo waliamua kumwadhibu kwa mujibu wa Sheria zao za Sungusungu za kumtaka awalipe shilingi laki tatu au ng,ombe  mmoja kwa ajili ya usumbufu na hasara ambayo wamepata kutokana na ucheweleshaji aliwasababishia, lakini baadae alikataa kutekeleza adhabu hiyo.
                          “Tumefurahi sana Mkuu wa Mkoa kufika hapo utatusaidia kutatulia tatizo la dawa hapa kwetu…tulimkamata  Mwakilishi wa KCCL Bw. Boface Kubiru akiwa ameficha  dawa za kuua wadudu katika pamba chupa 50 ,huku sisi hatuna dawa na tulikubaliana kumwadhibu kwa mujibu wa Sheria zetu za Sungusungu za kumpiga Masumule ya kulipa shilingi laki tatu au atulipe ng’ombe mmoja lakini alikataa…Mkuu Mkoa tunaomba utusaidie maana yeye ndiye alisababisha tuchelewe kupiga dawa na wadudu wakaongeza na kuanza kuharibu pamba yetu…tunaomba umsughulikie Mkuu” alisema Mwalemi.
                         Katika hatua nyingine Mkuu wa Mkoa wa Tabora amemwagiza Mkuu wa Polisi Wilaya  hiyo (OCD) kumkamata mumiliki wa Duka la kununua mazao mbalimbali aina ya karanga, mahindi na choroko linalojulikana kwa jina Kaliwa liliko Kitongoji cha Mkuyuni cha Kijiji cha Limbulasiasa kwa tuhuma za kununua mazao hayo kwa kutumia mzani wa rula uliopigwa marufuku kwa kuwa inatumika kuwanyonya wakulima.
                      Mkuu huyo wa Mkoa alichukua hatua hiyo baada ya kumkuta mfanyabiashara huyo akiendelea kutumia mzani huo licha ya kupigwa marufuku muda mrefu na Serikali kwa sababu umekuwa ukitumika kuwaibia wakulima.
                     Alimwagiza OCD kuhakikisha anakamata pia mzani wake na mhusika ili aweze kushitakiwa kwa mujibu wa Sheria.
Mkuu wa Mkoa wa Tabora anaendelea na ziara yake katika maeneo mbalimbali ya Mkoa huo ambayo yanayolima pamba kwa ajili ya kuwaelimisha wakulima wa zao hilo juu ya unyunyuziaji sahihi wa dawa za kuua wadudu.

Na Tiganya Vincent, Tabora

No comments:

Post a Comment