KWA MAONI AU USHAURI E-mail: inocomm2014@gmail.com, PIGA SIMU: 0714555668

www.utt-pid.org


TEMBELEA: www.utt-pid.org

December 23, 2014

MWANAHARAKATI AVAA GUNIA NA KUTINGA OFISI ZA JIJI KUMDAI MKURUGENZI WA JIJI LA MWANZA AMLIPE FEDHA ZAKE


Mwanaharakati John Masweta akiwa kwenye geti kuu la Makao Makuu ya Jiji la Mwanza.…




MKURUGENZI wa Jiji la Mwanza, Halifa Hassan Hida ameingia katika kashfa nzito baada ya mwanaharakati aliyefahamika kwa jina la John Masweta kutinga kwenye geti kuu la Makao Makuu ya Jiji la Mwanza jana huku akiwa amevaa gunia kumshinikiza mkurugenzi huyo amlipe shilingi 1,600,000 aliyopewa kama zawadi na uongozi wa mkoa na mkurugenzi huyo kushindwa kuilipa fedha hiyo kwa wakati.
Akizungumza na waandishi wa habari jijini Mwanza kwenye lango kuu la kuingia ofisi za jiji hilo, Masweta alisema kuwa yeye ni Mwanzilishi na Mkurugenzi wa Kampuni ya  Tanzania Environment & Conservation (TECO) aliyejitolea kwa zaidi ya miaka 20 kupanda miti na amekuwa akipewa tuzo mbalimbali kutokana na kazi hiyo na kuweza kuliokoa taifa katika majanga ya jangwa.
Masweta ameendelea kufafanua kuwa katika kuhakikisha analisaidia taifa, amepanda miti katika maeneo mbalimbali jijini Mwanza na wakati akiendelea kupanda miti hiyo akawa amepatiwa tuzo ya mwanaharakati bora kwa kutunza mazingira iliyoambatana na fedha taslimu shilingi milioni moja na laki sita lakini cha kushangaza mkurugenzi amekataa kutoa fedha hiyo na badala yake amempatia cheti tu bila kumpatia na fedha.
Katika hatua nyingine, Masweta ameendelea kusema kuwa yeye hakupanda miti kwa lengo la kulipwa na taifa bali alipanda miti ili kuliondoa taifa katika janga la kukumbwa  na jangwa lakini cha kushangaza kila anapotiwa moyo kwa kupatiwa fedha kidogo, fedha hiyo huishia mikononi mwa watu wengine ambao hawana huruma na maisha yake.
Hata hivyo, Masweta alikuwa na mabango yaliyoandikwa ujumbe mbalimbali kama  Toa nguvu zako kwa kulitumikia taifa, uwe faida kwa jamii na taifa,  onea huruma tumbo lako kula mpaka sisimizi, Udhalimu wa Mkurugenzi wa Jiji la Mwanza haukubaliki.
Masweta amesema kuwa hatoki kwenye lango hilo hadi pale mkurugenzi huyo atakapompatia kiasi hicho cha fedha anazodai.
Aidha Masweta ametoa rai kwa raia kwa kusema kuwa yeye ni mgonjwa wa kisukari na hajanywa maji yoyote tokea asubuhi endapo akifariki basi wafahamu kwamba aliyesababisha kifo chake ni Mkurugenzi wa Jiji la Mwanza kutokana na kuwa na nia ya kudhulumu haki za wenzake.

No comments:

Post a Comment