KWA MAONI AU USHAURI E-mail: inocomm2014@gmail.com, PIGA SIMU: 0714555668

www.utt-pid.org


TEMBELEA: www.utt-pid.org

April 3, 2015

ZITTO,UKAWA NGOMA NZITO

Mh. Zitto Kabwe
 Zitto aliyekuwa Mbunge wa Kigoma Kaskazini kwa tiketi ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), alitimuliwa kwenye chama hicho hivi karibuni na siku chache baadaye, akaibukia kwenye chama hicho na kuchaguliwa kuwa Kiongozi Mkuu Taifa wa chama hicho.
Baada ya uchaguzi huo, Machi 29, 2015, ACT kilizinduliwa rasmi katika hafla kubwa iliyoacha gumzo, iliyofanyika kwenye Ukumbi wa Diamond Jubilee jijini Dar es Salaam na kuwakutanisha watu mbalimbali kutoka mikoa kadhaa ya Tanzania sambamba na wageni waalikwa kutoka nje ya nchi.
Jeuri ya fedha iliyotumika kwenye uchaguzi huo, kwa kukodi ukumbi wa gharama, kuwagharamia wajumbe wote kutoka mikoani na kurusha matangazo ya runinga moja kwa moja kupitia runinga za ITV na Azam TV, ilisababisha minong’ono mingi kuanza kusambaa kwamba nyuma ya chama hicho, kulikuwa na mkono wa Chama Cha Mapinduzi (CCM).
“Haiwezekani chama ndiyo kwanza kimeanzishwa juzijuzi tu halafu wawe na jeuri ya fedha kiasi hiki, kurusha matangazo ya moja kwa moja kwenye runinga mbili za ITV na Azam TV kunagharimu fedha nyingi sana, Zitto na wenzake wamepata wapi fedha hizo? Kuna mkono wa mtu hapa,” mdau mmoja aliyeomba hifadhi ya jina lake, aliliambia Uwazi Mizengwe nje ya ukumbi huo wakati uzinduzi ukiendelea.
Wasomaji wengine waliofuatilia uzinduzi huo, walipiga simu chumba cha habari na kudai kuwa kuna zengwe limeandaliwa kumpaisha Zitto na chama chake kwa lengo la kupunguza kura za Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) katika uchaguzi mkuu ujao.
“Hawa jamaa (CCM) ni wajanja sana, wameamua kuwekeza ACT kwa kuwapa fedha na kuwagharamia kila kitu ili kuwachanganya wapinzani. Unajua mpaka sasa tayari kuna watu walikuwa Ukawa wameshahamia kwa Zitto, CCM wamefanya makusudi ili waendelee kutawala, wanatumia ile falsafa isemayo ‘Divide and Rule’ (Gawanya kisha Tawala),” alisema Sunday Makweta wakati akizungumza na gazeti hili.
Ili kupata ukweli wa zengwe hilo, Uwazi Mizengwe liliingia kazini ambapo lilianza kwa kumtafuta Zitto. Alipopatikana, alisomewa madai kwamba chama chake kinadaiwa kufadhiliwa na CCM kwa lengo la kudhoofisha Ukawa ambapo alishangaa madai hayo na kufunguka:
“Huyo anayetuhumu hivyo aseme huyo mfadhili ni nani na kafadhili nini. Yeyote mwenye mawazo hayo hafikirii. Wanachama wamejitolea, gharama za kurusha matangazo ya moja kwa moja tumepewa discounts (punguzo la bei). Tumechanga kutoka kwa marafiki, hiki chama ni sawa na moto wa pumba, ni chama kikubwa na tumedhamiria.”
Uwazi Mizengwe lilimtafuta pia mwenyekiti wa chama hicho (Taifa), Annastazia Mghwira alisema si kweli kwamba chama chao kinafadhiliwa na CCM kwa sababu kwanza wana kesi dhidi ya chama hicho mahakamani kutokana na madai ya kuibiwa kura kwenye uchaguzi wa serikali za mitaa.
“Chama chetu kinapaa kutokana na wanachama kujitolea na tunataka kuhamisha uwezo kwa wananchi na kuing’oa CCM madarakani.”

No comments:

Post a Comment