KWA MAONI AU USHAURI E-mail: inocomm2014@gmail.com, PIGA SIMU: 0714555668

www.utt-pid.org


TEMBELEA: www.utt-pid.org

June 23, 2015

HUYU NDIYE KAIMU MUFTI


Kaimu Mufti, Abubakar Zubeir
Baraza la Ulamaa limemchagua, Sheikh Abubakar bin Zubeir Ally, kuwa Kaimu Mufti Mkuu wa Tanzania katika kikao chake  kilichofanyika jana mjini Bagamoyo, mkoani Pwani.
Kwa mujibu wa Katibu Mkuu wa Baraza Kuu la Waislamu Tanzania (Bakwata), Sheikh Suleiman Lolila, Kaimu Mufti Zubeir alichaguliwa kwa kura za wajumbe wote wa baraza hilo.
“Kaimu Mufti amechaguliwa leo (jana) asubuhi na Baraza la Ulamaa linaloundwa na wajumbe saba katibu naye akishiriki amepata kura nane zilizompa ushindi,” alisema Sheikh Lolila.
Aidha, alisema baada ya kumchagua kaimu mufti huyo kitakachofuata ni kutengeneza mikakati ya kufanya uchaguzi mkuu wa Bakwata baada siku 90 ambao utashirikisha viongozi wa ngazi mbalimbali wa baraza hilo.
Alisema mkutano huo mkuu ndiyo utakaomchagua Mufti Mkuu mpya ataziba  nafasi ya Sheikh Mkuu Mufti, Issa Shabani Simba, aliyefariki dunia Juni 15, mwaka huu katika Hospitali ya TMJ jijini Dar es Salaam.
MATARAJIO YAKE
Kwa upande wake, Kaimu Mufti Mkuu, Sheikh Zubeir bin Ally, alisema matarajio yake ni kuendeleza mambo aliyoacha Marehemu Mufti Simba.
“Matarajio yangu ni kuendeleza yote aliyofanya na aliyoacha Mufti Simba ikiwa pamoja na kuanzisha mapya,” alisema Sheikh Ally.
Kaimu Mufti Ally alisema katika kipindi chake cha kukaimu atajenga mshikamano kati ya waislamu pamoja na kushirikiana na viongozi wa Baraza la Ulamaa kwa ajili ya kuboresha na kuimarisha uhai wa baraza hilo.
Alisema atakuwa tayari kupokea ushauri utakaosaidia kuijenga Bakwata na kwamba ni matarajio yake ni kuifanyia marekebisho Katiba ya baraza hilo iliyokuwa ikilalamikiwa muda mrefu kwa kushirikiana wajumbe, katibu na watendaji ili iweze kukidhi matakwa ya Waislamu wote.
Aliwataka waumaini wa dini ya Kiislam na jamii kwa ujumla kuendelea kulinda na kudumisha amani ili nchi iendeelee kuwa mahali pazuri na salama kuishi na watu kuabudu.
DK. SLAA AMTEMBELEA
Katibu Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Dk. Willibroad Slaa, amemtembelea nyumbani kwake Kaimu Sheikh Mkuu, Mufti Abubakar bin Zubeir Ally, kumpongeza na kumtakia majukumu mema akimhakikishia ushirikiano kama jirani na kiongozi.
Sheikh Zuber atakaimu nafasi hiyo ya juu kwa siku 90 hadi hapo atakapochaguliwa Mufti Mkuu kwa mujibu wa katiba ya Baraza Kuu la Waislamu Tanzania (Bakwata). 
Zubeir anaishi mtaa wa Ufipa, Kinondoni, jijini Dar es Salaam, jirani na zilipo ofisi za Makao Makuu ya Chadema.
Mbali ya kumtakia kila la heri, Dk. Slaa alimuahidi Mufti Sheikh Zuberi kuwa Chadema iko tayari wakati wowote kutoa ushirikiano atakaouhitaji katika kutimiza wajibu wake huo.
 “Nitumie fursa hii pia kusema tukiwa majirani zako hapa Mtaa wa Ufipa, tukiwa viongozi ambao tunao wanachama, wapenzi na wafuasi wetu wenye dini tofauti wakiwamo Waislam, naomba kukuhakikishia ushirikiano kutoka kwetu wakati wowote katika kutimiza majukumu yako haya makubwa na nyeti,” alisema. Mufti Simba alizikwa Juni 16, mwaka huu katika makaburi ya Nguzo Nane, mkoani Shinyanga, mazishi yake yakiongozwa na Rais Jakaya Kikwete na kuhudhuriwa mamia ya wananchi wakiwamo viongozi wa serikali, dini na vyama vya siasa. 
Sheikh Mkuu mpya wa Tanzania atapatikana miongoni mwa wajumbe wa Baraza la Ulamaa linaundwa na Kadhi Mkuu, Sheikh Abdallah Mnyasi na naibu wake Sheikh Ali Muhidin Mkoyogole.
Wengine ni Sheikh wa Mkoa wa Mwanza, Salum Fereji, Sheikh wa Mkoa wa Shinyanga, Ismail Makusanya, Sheikh wa Mkoa wa Kigoma, Hassan Kiburwa na Kadhi wa Mkoa wa Dar es Salaam, Sheikh Hamid Masoud Jongo.

No comments:

Post a Comment