Na Jacquiline Mrisho- maelezo
Idadi ya wagonjwa wa kipindupindu jijini
Dar es salaam imepungua kufikia wagonjwa kumi na mbili (12) kwa mkoa
mzima, huku wilaya ya Temeke ikiwa na wagonjwa saba,Kinondoni wagonjwa
wanne na Ilala ikiwa na mgonjwa mmoja
.
Haya yamezungumzwa na Mratibu wa Magonjwa
ya kuambukiza wa Jiji la Dar es salaam Bw. Alex Mkamba ofisini kwake
leo akielezea jinsi gani mkoa umefanikisha kupambana na kipindupindu kwa
kuzingatia usafi katika jiji.
Ameongeza kuwa katika kufanikisha mapambano
dhidi ya kipundupindu wametoa mafunzo juu ya mbinu shirikishi ya namna
ya kujikinga na kipindupindu kwa watendaji wa mitaa na pia imewahimiza
kukagua maeneo yao na kuwapa kibali cha kufunga maeneo ya biashara au
maeneo yatoayo huduma za chakula yasiyozingatia usafi.
Akielezea kuhusu huduma kwa wagonjwa wa
kipindupindu jijini Dar es salaam mratibu huyo amesema jiji lina dawa
za kutosha za kuhudumia wagojwa ipasavyo kwa kuwapatia huduma bora
zaidi kuendana na kasi ya maambukizi yaliyopo.
“ hata leo Shirika la Afya Duniani (WHO)
limetoa dawa za kusafishia maji (Water Guard) maboksi 45 kwa kila
wilaya” Mkamba alifafanua.
Aidha alisema serikali imejipanga katika
kudhibiti maambukizi mapya kwa kuwapima wagonjwa kabla na baada ya
kuruhusiwa kutoka hospitalini na aliwashauri wananchi kubadili tabia
kwa kuhakikisha usafi unafanyika pia kuchemsha maji na kuufanya usafi
kuwa ni tabia yao ya kila siku.
Mpaka sasa jumla ya watu 55 wamefariki dunia kwa ugonjwa wa kipindupindu jijini Dar es salaam.
No comments:
Post a Comment