KWA MAONI AU USHAURI E-mail: inocomm2014@gmail.com, PIGA SIMU: 0714555668

www.utt-pid.org


TEMBELEA: www.utt-pid.org

May 18, 2016

SERIKALI KUWAWEZESHA WANANCHI KUPATA TAARIFA NA HUDUMA MBALIMBALI KUPITIA SIMU ZAO.

Picha na 3
Mtendaji Mkuu wa Wakala ya Serikali Mtandao (e-Government Agency) Dkt. Jabiri Bakari akiwa katika moja ya majukumbu yake.
……………………………………………………………………………………………………
Na. Aron Msigwa – MAELEZO.
SERIKALI kupitia wakala ya Serikali mtandao imesema kuwa inaendelea kulifanyia kazi suala la uanzishaji wa mfumo wa TEHAMA utakaowawezesha wananchi kupata huduma na taarifa mbalimbali za Serikali kupitia simu zao mkononi mahali popote walipo kwa njia ya mtandao.
Utaratibu huo pia utawawezesha wahitimu wa vyuo mbalimbali vya elimu nchini Tanzania kupata taarifa za ajira za Serikali na kuwawezesha kuomba nafasi hizo, kufuatilia majibu ya usaili  walioufanya na kupata taarifa za kuitwa kazini kupitia namba za utambulisho watakazopewa kupitia ujumbe mfupi (sms).
Akizungumza na Wahariri wa vyombo vya Habari leo jijini Dar es salaam Mtendaji Mkuu wa Wakala ya Serikali Mtandao (e-Government Agency) Dkt. Jabiri Bakari amesema kuwa   mfumo huo utamuwezesha mwananchi kupata huduma za Serikali mahali popote alipo kufuatia mifumo ya TEHAMA kuwasiliana na kubadilishana taarifa.
Amesema kuwa dhana ya Serikali Mtandao  ni kuwa na matumizi ya TEHAMA kwenye shughuli zote za Serikali kwa lengo la kuongeza ufanisi na kupunguza gharama za uendeshaji kwenye huduma za Afya, Utalii, Malipo ya tozo za huduma,vibali, leseni ,elimu na huduma mbalimbali za Serikali.
Dkt. Jabiri amesema  moja ya vitu vinavyosababisha usumbufu kwa wananchi kutokana na kukosekana kwa Serikali mtandao ni pale wanapohitaji kupata huduma za Serikali ikiwemo Hati ya kusafiria ambapo hulazimika kwenda Idara ya Uhamiaji kujaza fomu maalum na kisha kusubiri kwa muda wa zaidi ya wiki moja ili taarifa zao ziweze kuhakikiwa na taasisi nyingine za Serikali wakati suala hilo lingeweza kuchukua siku moja.
“Matumizi ya TEHAMA kwenye shughuli za Serikali hurahisiaha sana upatikanaji wa taarifa  kwa kuwa mifumo inawasiliana na kubadilishana taarifa haimlazimu mwananchi kwenda kwenye taasisi zaidi ya tano kupata huduma yake” Amesisitiza Dkt. Jabiri.
Amesema taasisi za Serikali kama Jeshi la Polisi, Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA), Idara ya Uhamiaji, RITA na taasisi nyingine ambazo majukumu yao hutegemeana kupitia serikali mtandaomifumo ya taasisi hizo huunganishwa ili ifanye kazi pamoja kwa lengo la kuruhusu mifumo kuzungumza  kumuhudumia mwanachi bila yeye kulazimia kuzifuata taasisi hizo.
Amesema kuwa pamoja na maboresho mbalimbali yanayoendelea ndani ya Serikali ya  kujenga Serikali mtandao imara mfumo uliopo sasa kwenye baadhi ya taasisi humfanya mwananchi achukue muda mrefu kupata huduma.
Ameeleza kuwa taasisi za Serikali zinazofanya kazi katika mazingira yanayofanana zinaposhirikiana katika kutoa huduma Kupitia Serikali mtandao mwananchi wa kawaida hatajua nini kinaendelea, atakachokipata mwisho ni majibu ya huduma aliyoiomba kama ni  Bandarini atachukua mzigo bila usumbufu wowote kwa kuwa suala la kodi, upakuaji na upakiaji wa mizigo na ukaguzi halitamgusa mwananchi.
Ameongeza kuwa ili Serikali mtandao iweze kufanya kazi yake ipasavyo nchini lazima kuwe na miundombinu ndani ya taasisi au nje pia uwepo wa mifumo Tumizi ( Application Systems) inayoshughulikia masuala mbalimbali, wafanyakazi pamoja na Sera, miongozo na taratibu za kusimamia TEHAMA  kuwezesha huduma mtandao ( e – Servieces).
Dkt. Jabiri amesisitiza Tanzania iko kwenye hatua ya kwanza na ya pili, kwa maana ya taasisi nyingi za Serikali zina tovuti zenye taarifa za awali za kumsaidia mtu kujua nini kinapatikana au kutolewa na taasisi za serikali ili aweze kuchukua hatua ya kupata huduma.
Amesema Wakala ya Serikali mtandao imefanikiwa kuweka mifumo kwa maana ya Tovuti kuu ya Serikali, Tovuti ya Wananchi, Tovuti ya data huria ambayo ina taarifa mbalimbali za wananchi kuhusu Maji, Barua pepe ya Serikali (GMS) ambayo sasa inatumiwa na jumla ya taasisi 117 za Serikali na Balozi mbalimbali kwa lengo kuepuka matumizi ya barua pepe za muda.

No comments:

Post a Comment