KWA MAONI AU USHAURI E-mail: inocomm2014@gmail.com, PIGA SIMU: 0714555668

www.utt-pid.org


TEMBELEA: www.utt-pid.org

August 19, 2016

SERIKALI YAPIGA MARUFUKU BIASHARA HOLELA YA MKAA

WIZARA ya Maliasili na Utalii kupitia Huduma za Misitu Tanzania ( TFS) imepiga marufuku usafirishaji wa mazao ya misitu ikiwemo mkaa ambapo mfanyabiashara anayefanya biashara hiyo, atapaswa kuwa na vigezo ambavyo Serikali inavihitaji, tofauti na hapo sheria itachukua mkondo wake.

Imesema zuio hilo linakwenda sambamba na kupiga marufuku usafirishaji wa magogo ya miti kwenda nje ya nchi, magari kubeba mbao yakiwa yamefunikwa, pikipiki na baiskeli kubeba mkaa kwenda sehemu moja hadi nyingine mijini na vijijini.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam juzi, Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Misitu Tanzania (TFS), Profesa Dos Santos Silayo, alisema uamuzi huo ni moja ya mikakati ya kukusanya maduhuli stahiki ya rasilimali za misitu na kuwabana wakwepa ushuru.

Alisema moja ya majukumu ya TFS, ni kuhakikisha inaanzisha na kusimamia rasilimali za misitu ili zisaidie ustawi wa taifa kwa kizazi cha sasa na kijacho, hivyo ni lazima wananchi wafahamu kuwa ni kosa kuvuna hovyo misitu na bidhaa zake bila kibali.

Mtendaji huyo alisema kila zao linalotokana na misitu ni lazima lilipiwe ushuru stahiki na kukatiwa risiti, hivyo kukwepa kufanya hivyo kwa kutumia njia mbalimbali zinazokatazwa ni kuvunja sheria na kuiibia serikali mapato.

“Mazao ya misitu, ikiwemo mikaa ni kosa kuuzwa na kusafirishwa bila kuwepo kibali na risiti. Muuza mkaa lazima uwe na risiti, na wewe mnunuzi tukikukamata na gunia la mkaa na huna risiti utawajibika.

“Tunataka kuhakikisha maduhuli ya mazao ya misitu yanakusanywa ili kupata matumizi endelevu ya rasilimali za misitu hivyo ni biashara hii ya miti, mkaa na mazao ya nyuki inatakiwa iwe wazi.

“Ni marufuku kusafirisha mazao ya misitu usiku, kama mtu ana vigezo vyote tunavyovihitaji kusafirisha mazao ya misitu anatakiwa kusafiri kuanzia saa 12 asubuhi mpaka saa 12 jioni, ikipita hapo, weka pembeni gari mpaka asubuhi,” alisema.

Aidha alisema TFS chini ya Wizara ya Maliasili ina Meneja miti kwenye kila wilaya, ambao wanafanya kazi kwa karibu na Maofisa Watendaji wa vijiji ambao hushirikiana kutoa vibali kwa kuvuna miti stahiki kisheria na kutoa risiti.

Alisema risiti hizo pamoja na vigezo vingine ikiwemo kuwa na usajili wa TFS, leseni ya biashara na namba ya utambulisho wa mfanyabiashara (TIN), hati ya kusafirisha mazao ya misitu humfanya mfanyabiashara kuruhusiwa kuendelea na biashara ya mazao ya miti nchini.

Profesa Silayo alisema TFS wataendelea na majukumu yao kwa ufanisi ikiwa ni pamoja na kutekeleza maagizo yaliyotolewa na Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa, alipozungumza na watumishi wa wizara hiyo mapema mwezi uliopita.

No comments:

Post a Comment