Benny Mwaipaja, WFM-Dodoma
Serikali imesema kuwa
mabadiliko ya sekta ya fedha ya mwaka 1991 yalipelekea Serikali kujitoa
katika uendeshaji wa moja kwa moja wa shughuli za kibenki nchini ili
kuruhusu mfumo wa Soko Huria, hususan nguvu ya soko kuamua viwango vya
riba za mikopo, riba za amana na gharama zingine za huduma za kibenki.
Kauli hiyo imetolewa Bungeni
mjini Dodoma na Naibu Waziri wa Fedha na Mipango (MB), Mhe. Dkt. Ashatu
Kijaji, alipokuwa akijibu swali la msingi la Mbunge wa Viti Maalumu
Mhe. Jesca David Kishoa (CHADEMA), aliyehoji licha ya kuwa na benki
nyingi zaidi kuliko nchi zote Kusini na Mashariki mwa Afrika, kwa nini
wingi huo bado haujaleta unafuu katika tozo ya riba.
Akijibu swali hilo Mhe. Dkt.
Kijaji alisema kuwa, viwango vya riba za mikopo hupangwa kwa kuzingatia
gharama za upatikanaji wa fedha, uendashaji, bima, sifa za mkopaji na
hatari ya mkopaji kutolipa mkopo, pamoja na kasi ya mfumuko wa bei.
“Dhana ya uhitaji na utoaji wa mikopo siyo kigezo pekee
kinachoweza kupunguza viwango vya riba hapa nchini, hatari ya kutolipa
mkopo ni kigezo kikubwa kinachotumiwa na benki kupanga viwango vya riba
za mikopo, hususan kwa wajasiriamali wadogo”. Alisema Dkt. Kijaji
Dkt. Kijaji aliongeza kuwa, uzoefu
uliopo unaonesha kuwa, benki zinapendelea kukopesha wajasiriamali
waliojiunga katika vikundi kuliko mjasiriamali mmoja mmoja ili kupunguza
kiwango cha mikopo isiyolipika.
Aidha, Mbunge wa Viti Maalumu Mhe. Jesca David Kishoa, alihoji
ni kwa nini Serikali isiweke ukomo wa riba kisheria kwa benki hizo ili
kumsaidia mjasiriamali wa sekta binafsi kama ilivyofanya nchi ya Kenya.
Dkt. Kijaji alifafanua kuwa, kwa mujibu wa Sheria ya Taasisi
za Fedha ya Mwaka 1991, iliyotungwa kwa kuzingatia misingi ya mfumo wa
soko huria, Benki Kuu imepewa jukumu na mamlaka ya kusimamia na
kuzichukulia hatua taasisi za fedha zinazoendesha shughuli zao kwa
hasara.
Aliongeza kuwa, kutoa maelekezo kwa benki kutumia viwango
fulani vya riba, kutaifanya Benki Kuu kukosa nguvu na mamlaka ya
kuzichukulia benki hatua endapo zitapata hasara kwa kutumia riba ambayo
Benki Kuu imeelekeza.
Katika swali la nyongeza Mbunge
huyo, alieleza kuwa mikopo isiyolipika imekua kwa kiwango kikubwa tangu
mwaka 1991 huku akitaja sababu kubwa mbili ambazo ni mazingira magumu ya
biashara pamoja na riba kubwa kwa wafanyabiashara hao.
‘’Je Serikali haioni umuhimu wa
kuwasaidia kwa kuwapa riba nafuu ili iweze ‘Kustimulize’ (kuchochea)
biashara zao’’. Alihoji Mhe. Kishoa.
Akijibu swali hilo la nyongeza
Naibu Waziri wa Fedha na Mipango, Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji alisema kuwa
kutokana na mabadiliko ya mfumo wa mwaka 1991 ya sheria ya Mabenki na
Taasisi za fedha, Benki Kuu au Serikali haiwezi kutoa mweleko au ukomo
wa Taasisi za fedha.


No comments:
Post a Comment