Spika
wa Bunge, Job Ndugai jana Alhamisi amegomea Serikali na kulazimika
kuahirisha Bunge kwa muda wa saa moja ili warudi na kukubaliana kubadili
jina la Shirika la Wakala wa Meli wa Taifa (NASAC)
Spika
Ndugai alitoa agizo la kuahirisha Bunge baada ya mvutano wa Serikali na
Kamati ya Bunge ya Miundombinu ambao walipendekeza kubadilishwa kwa
jina hilo.
Mapema
wakati Serikali ikijibu maoni ya wabunge kuhusu muswada huo, Spika
alionyesha dhahiri kutokukubaliana na wazo la Serikali na badala yake
akasimama katika mawazo ya kamati na wabunge wengine kuwa jina hilo
halifai.
Mara
baada ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, George Masaju kumaliza yake,
Spika alihoji ni kwa nini asikubaliane na mapendekezo ya wabunge katika
kubadili jina la muswada lakini mwanasheria huyo akatupia mpira kwa
waziri kuwa angekwenda na majibu.
Hata
hivyo, katika majumuisho ya michango ya wabunge, Waziri Profesa Makame
Mbarawa alitoa sababu za kutobadilisha jina akisema halikuwa na maana
yoyote na wala lililopendekezwa halikuwa na madhara kwani waliosema kuwa
jina hilo ndilo lililofilisi hawakujua kuwa kulikuwa na usaliti.
“Mheshimiwa
Spika, jina halina shida yoyote kwani hata lile la awali siyo kwamba
lilipeleka madhara bali kilichotokea ni namna ambavyo baadhi ya watu
waliokuwa ndani ya chombo hicho walikuwa ni wasaliti,” alisema Mbarawa
Baada
ya hoja za waziri huyo Bunge lilikaa kama kamati na kuanza kuangalia
vifungu hivyo ndipo Spika akampa nafasi mwenyekiti wa kamati hiyo
Profesa Norman Sigala ambaye akasema Serikali ilikuwa imewadanganya.
“Nakushukuru
mheshimiwa Spika, Serikali hapa ni kama imetudanganya maana kusema
itaangalia huko mbeleni ni sawa na kutudanganya sisi, tulichokubaliana
kwenye kamati sicho kilichowasilishwa bungeni,” alisema Profesa Sigala.
Spika
alimpa nafasi Waziri ambaye aliendelea kuweka msimamo kuwa jina hilo
liendelee kama lilivyowasilishwa na Serikali ili kama kutakuwa na
marekebisho mbeleni Serikali itafanya hivyo.
Kauli
ya waziri ilimuinua Spika ambaye alisema jina hilo linapeleka picha
mbaya kwani haiwezekani Serikali kuunda chombo kipya kizuri lakini
ikatumia jina ambalo lina maudhui mabovu.
“Hapa
ndipo tunatunga sheria yenyewe, sasa kama mnaona kubadili jina kunaweza
kuathiri kisheria niambie lakini kama hakuna, sioni kwa nini tuendelee
kuvutana sana, naahirisha shughuli za Bunge kwa saa moja nendeni katika
ukumbi wangu hapo mkutane na mjadiliane ili mkirudi hapa mniletee jina,”
alisema Spika na kuahirisha Bunge
Wabunge
walilipuka kwa makofi na makelele ya kumshangilia Spika huku wanasheria
wakikutana kwa haraka ambapo Mwanasheria Mkuu wa Serikali na Waziri wa
Katiba na Sheria, Profesa Palamagamba Kabudi waliwaongoza wajumbe wa
kamati na serikali haraka kuingia ukumbini kwa ajili ya kutafuta jina
hilo.
No comments:
Post a Comment