KWA MAONI AU USHAURI E-mail: inocomm2014@gmail.com, PIGA SIMU: 0714555668

www.utt-pid.org


TEMBELEA: www.utt-pid.org

March 23, 2018

SAKATA LA KOROSHO YA TANZANIA KUKUTWA NA KOKOTO VIETNAM KUSOMBA WENGI.......WAZIRI TIZEBA ATOA MAAGIZO MAZITO KWA IGP

                  Waziri wa Kilimo, Dk. Charles Tizeba, ameagiza kuwasilishwa kwa Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini (IGP) orodha ya watu wote waliohusika katika sakata la korosho za Tanzania zilizokutwa na kokoto nchini Vietnam ili wakamatwe na kuhojiwa.
                Hata hivyo, amesema taarifa zinasema jambo hilo si la kwanza kufanyika nchini. Dk. Tizeba alitoa agizo jana baada ya kuwasilishwa taarifa ya uchunguzi korosho hizo iliyotolewa na kamati iliyoundwa kuchunguza suala hilo.
               Akizungumza baada ya kupokea ripoti hiyo, Dk. Tizeba alimuagiza Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Mathew Mtigumwe, kuwasilisha orodha hiyo kwa IGP ili hatua stahiki zichukuliwe dhidi yao.
                   “Waende sasa wakahojiwe rasmi na vyombo vya dola, naomba hili lifanyike leo (jana) ili wahojiwe kwamba wewe fulani ulikuwa mahali fulani wajibu wako ulikuwa huu hukufanya hivyo, na kama wakibainika wana kesi ya kujibu sheria ichukue mkondo wake,” aliagiza Tizeba.
                    Alisema katika ripoti hiyo kuna majina ya watu waliohusika katika kusimamia shughuli yote ya usafirishaji wa korosho kuanzia iliponunuliwa, makampuni ya usafirishaji, waliofanya ubadilishaji kwenye shirika la meli nchini (Nassaco).
                    “Majina yao yamo na Ofisa wa Serikali wa Mamlaka ya Mapato (TRA) aliyetakiwa aweke ‘seal’ kwenye hizo kontena kwa wakati baada ya kuwekwa kwenye magunia ili kujiridhisha kwamba alichokishuhudia kinawekwa kwenye kasha hakitabadilishwa na kuweka lakiri ya serikali kwamba humo ndani kuna mzigo uko ndani ya udhibiti wa forodha, huyu naye anafahamika kwa jina,” alisema.
                  Alisema kwanini baada ya kufungwa makontena hayo yalibaki kwa siku tano hadi sita yawezekana hakukuwa na meli ya kusafirisha, lakini yale ya kusafiri yanakwenda yanapata nafasi kampuni ya kimataifa ya kuhudumia Shehena za makontena Bandarini (TICTS) ambapo makontena ambayo yamefika huwa yanatoka kupisha yanayosafirishwa.
             “Tutajua huyu naye ni nani ambaye pia yumo humu ambaye alitakiwa kuyatoa Nassaco kuyapeleka Ticts na TPA (Mamlaka ya Bandari), tutataka tujue hayo mambo nyie haikuwa kazi yenu kuchukua hatua, kazi yenu ilikuwa ni kukusanya taarifa,” alisema Tizeba.
               Alisema ubalozi wa Vietnam ulifikisha serikalini malalamiko rasmi kuhusu mawe yaliyopatikana kwenye viroba vya korosho nchini humo.
                “Mimi binafsi niliongea naye na akanionyesha kwa namna mbalimbali jinsi wafanyabiashara wa Vietnam walivyokuwa wamepokea korosho zilizochanganyika na vitu mbalimbali ikiwamo mawe,” alisema Tizeba.
             Alieleza kuwa taarifa ya Balozi ilionyesha korosho imenunuliwa mkoani Lindi, lakini akitazama mawe yaliyokuwamo sio ya Nachingwea au Liwale kunakopatikana mwambao wa pwani.
             Alibainisha pia jambo jingine ambalo limeendelea kujitokeza ni kuwapo kwa mchanga kwenye magunia ya korosho na siku nne zilizopita imegundulika kontena moja lilikuwa limechanganywa na mawe katika Bandari ya Dar es Salaam.
                 Dk. Tizeba alisema mtu amenunua tani 20 za Korosho zinaondolewa tani 3 au 1.5 badala yake yanaingizwa mawe au mchanga na michikichi.
             Alisema atampatia ripoti hiyo Waziri wa Ujenzi, Mawasiliano na Uchukuzi, Prof. Makame Mbarawa, ili aweze kuona mambo yanayohusu wizara anayosimamia na kama kuna uwezekano wa kuboresha ufanyike.
                “Pia taasisi zingine za serikali zinazohusika na masuala haya ambapo kuna maghala yanayosimamiwa na Wizara ya viwanda na biashara nitampa hii ripoti Charles Mwijage,” alisema.
             Alisema kwa upande wa serikali wanaendelea na jitihada kupitia Wizara ya Mambo ya Nje na kwamba leo au kesho watakutana na wabunge kutoka Vietnam.
             “Tutakutana nao tuzungumze hili suala la korosho tuliweke vizuri, tumekutana na Balozi ambaye kasema wabunge hao wapo nchini na wangependa na wao kusikia.Tulikuwa tunasubiri ripoti yenu ilituwape picha kamili" Alisema

Kilichomo ndani ya Ripoti
                Makamu Mwenyekiti wa kamati hiyo, yenye wajumbe tisa Khasim Mbofu, alisema makontena yaliyokutwa na kokoto hizo ni kutoka Tanzania na pia limekutwa kontena bandarini lenye mchanga badala ya korosho likisafirishwa kupelekwa nchini humo.
                 Alisema kamati ilipata uhakika kuwa makontena hayo yalitokea Newala mkoani Mtwara na viashiria vikubwa vinaonyesha zilitoka Tanzania.
                  “Uthibitisho ni namba ya kontena ambazo zilikutwa kule zipo katika kumbukumbu ya bandari ya Dar es Salaam na bandari ya Nassaco, pia walibaini si jambo geni kutokea nchini na kwamba vyama vya ushirika vya msingi vya Pangateni, Mnyawi na Nguvumoja na Mkiu navyo vimeshawahi kukutwa na tatizo hilo,” alisema.
                Alieleza wakiwa bandarini walipata habari kuwa kuna kontena ambalo lilidhaniwa kuwa lina korosho zinazopelekwa Vietnam limebainika kuwa lina maboksi ya mchanga.
            “Tumeenda kuona kontena lilosadikika kuwa liliwekwa korosho zilizobanguliwa kwenda nchini Vietnam badala yake yamejaa mchanga na hili lilibainika katika scanner,” alisema.
                  Alisema walibaini baada ya korosho zilizokutwa na kokoto kuhamishwa kutoka katika malori na kwenda katika makontena ilichukua siku nne kufunga lakiri.
               “Eneo jingine la viashiria vya mchezo huu ni kwamba ulichezwa nchini kwa kuwa kontena hizi ilichukua siku 10 kutolewa bandari kavu ya Nassaco kwenda TICTS,” alisema.
                 Kadhalika, alisema wamebaini kuna mianya kati ya ghala kuu na bandarini na hakuna ulinzi wa kudhibiti.
                 “Tumetembelea mikoa ya Dar es Salaam, Pwani, Mtwara, Lindi, maghala na viwanda vya kubangua korosho na kufanya mahojiano na watu mbalimbali ukiwamo ubalozi wa Vietnam,” alisema.

Mapendekezo
                   Makamu huyo alisema vyombo vya uchunguzi vifanye uchunguzi wa kina kuhusu bandari ya Nassaco ambako ndiko korosho hizo zilitolewa katika malori na kuwekwa katika makontena kubaini uhalisia wake.
               Pamoja na hayo, alishauri Serikali ifunge scanner yenye nguvu itakayoweza kubaini kilichomo ndani ya magunia ikiwa ndani ya kontena na pia walibaini kuwepo kwa uhaba wa vitendea kazi katika bandari kavu ya Nassaco kutokana na kuwapo kwa malori mawili badala 12.
                Alisema kamati ilishauri kupitiwa upya kwa sheria ya korosho na kanuni zake zipewe upya ili ziendane na biashara ya zao hilo na pia kufungwa kwa mizani katika bandari kavu ya Nassaco.
                “Pia bandari ya Mtwara iboreshwe ili kuwa na uwezo wa kusafirisha korosho inayozalishwa katika mikoa ya kusini, na Serikali ihakikishe Mkoa wa Pwani unaingia katika mfumo wa stakabadhi ghalani kwa sababu katika hizo korosho zilizokutwa Vietnam kuna gunia 10 pia mbazo zilikutwa na chikichiki,” alisema.
            Aliongeza: “Yaani michikichiki inalimwa Kigoma sasa inakuwaje unakuta katika korosho?” alihoji.

No comments:

Post a Comment