
Hayo yameelezwa Bungeni Mjini Dodoma na Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira, January Makamba wakati akiwasilisha Azimio la Bunge la kuridhia makubaliano ya mkataba huo.
“Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuweka saini makubaliano hayo na hatimaye kuyatekeleza itanufaika na mambo mbalimbali ikiwemo kuimarisha hali ya uchumi wa nchi na kujenga uchumi endelevu wa viwanda wenye kustahimili mabadiliko ya tabianchi,” alisema Makamba.
Makamba Amesema, Mkataba huo utaongeza upatikanaji wa fursa zilizopo za miradi na teknolojia safi itakayowezesha matumizi ya gesi asilia majumbani na viwandani ili kuchochea maendeleo ya viwanda kwa kutumia nishati yenye bei nafuu.
Vilevile, utaimarisha ushirikiano baina ya Tanzania na Jumuiya ya Kimataifa katika kusimamia na kutekeleza masuala yanayohusu mabadiliko ya tabianchi.
“Makubaliano ya Paris yanalenga kuboresha utekelezaji wa Mkataba wa Mabadiliko ya Tabianchi wa mwaka 1992 kwa kutunza misitu inayonyonya joto, kuandaa na kutekeleza mipango ya kuhimili mabadiliko ya tabianchi na kuwa na mifumo ya upatikanaji wa fedha na teknolojia safi kwa nchi zinazoendelea ili kukabiliana na changamoto ya tabianchi,” alifafanua Makamba.
Aidha amesema, kwa kuzingatia manufaa yatokanayo na Mkataba huo pamoja na itifaki yake kwa Tanzania na pia umuhimu na manufaa ya makubaliano hayo, Bunge katika Mkutano wake wa Kumi na Moja na kwa mujibu wa Ibara ya 63 (3)(e) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977, linaazimia kuridhia makubaliano ya Paris kuhusu kuboresha utekelezaji wa Mkataba wa mabadiliko ya Tabianchi yaani “THE PARIS AGREEMENT UNDER THE UN FRAMEWORK CONVENTIN ON CLIMATE CHANGE”.
Na Lilian Lundo – MAELEZO, Dodoma


No comments:
Post a Comment