Mratibu
wa Mafunzo ya kuwajengea Uwezo Watendaji wa Bodi ya Chakula, Dawa na
Vipodozi, Patrick Mwesigye, kutoka nchini Rwanda, akitoa nasaha zake kwa
Watendaji hao katika uzinduzi wa mafunzo hayo katika Ukumbi wa Hoteli ya
Ocean View.
Mgeni rasmi Msajili wa Bodi ya Chakula, Dawa na Vipodozi Zanzibar, Dkt.
Burhan Othaman Simai (katikati), waliokaa akiwa katika Picha ya pamoja na washiriki wa mafunzo ya siku tano ya kuwajengea uwezo watendaji wa
Bodi ya Chakula, Dawa na Vipodozi, ambayo yanalenga kuanzisha Chombo
maalum cha pamoja cha Usajili wa Dawa katika nchi Wanachama wa Afrika
Mashariki.
Na Mwandishi wetu.
Jumuiya ya Afrika Mashariki
imeandaa Mafunzo ya kuwajengea uwezo Watendaji wa Bodi ya Chakula, Dawa
na Vipodozi Zanzibar ikiwa ni Mkakati wa kuunda Chombo maalum cha
pamoja cha usimamizi na usajili wa Dawa utakaofanywa katika nchi
Wanachama wa Jumuiya hiyo.
Mafunzo hayo ya siku tano
yanalengo la kuweka Msimamo wa Pamoja na Viwango sawa kwa Bodi za
Vyakula na Dawa ili Dawa itakaposajiliwa katika nchi moja ikubalike
kimatumizi katika nchi wanachama wa Afrika Mashariki.
Akizungumza katika uzinduzi wa mafunzo hayo katika ukumbi wa Hoteli ya Ocean View Msajili wa Bodi ya
Chakula, Dawa na Vipodozi Zanzibar, Dkt. Burhan Othaman Simai, amesema
kuwepo kwa chombo cha usimamizi wa pamoja katika nchi hizo kutasaidia
kuondokana na tatizo la uingizwaji wa Dawa zisizofaa Kimatumizi katika
nchi hizo.
Amesema, hombo hicho kitasaidia
kwa kiasi kikubwa kupunguza tatizo hilo kwa vile kutakuwa na mikakati ya
kupeana taarifa za karibu kuhusu Dawa zinazosajiliwa na kusambazwa
katika nchi zao.
Kwa upande wake Mratibu wa Mafunzo
hayo, Patrick Mwesigye, kutoka nchini Rwanda, amesema malengo ya jumuiya
hiyo ni kuhakikisha vitengo vyote vya nchi wanachama vinajengewa uwezo
na ufanisi ili viwe katika ubora unaofanana.
Amesema kwa sasa kila nchi
inatathmini na kusajili Dawa kivyake na kwamba kukamilika kwa mafunzo
hayo itakuwa ni hatua kubwa ya kufikia makubalianao ya kuanzishwa kwa chombo kimoja cha usajili wa Dawa katika nchi wanachama wa Afrika
Mashariki.
Akizungumza pembeni ya Mkutano huo
Mratibu mwenza kutoa Zanzibar, Hidaya Juma Hamad, amesema kukamilika kwa chombo hicho kutasaidia sana upatikanaji wa Dawa salama katika nchi
husika.
Amesema sambamba na hilo kutasaidia kupunguza gharama na matumizi mengi ya rasilimali ambayo yangetumika katika nchi zingine.
“Dawa moja kuisajili inaweza
kuchukua miaka miwili kwa hiyo Dawa hiyo itakaposajiliwa katika nchi
moja itakuwa na uhalali wa kutumika katika nchi nyingine bila kusajiliwa
tena, na hapo gharama kubwa zitakuwa zimeepukwa” Alisema Hidaya.
Pamoja na Zanzibar kupewa mafunzo
hayo bado inakabiliwa na Changamoto nyingi zinazokwaza ufanisi wao
ikiwemo uhaba wa Fedha, Ofisi ndogo na idadi ndogo ya wataalamu na watendaji wa kukagua maduka ya Dawa, Vyakula na upekuzi bandarini.




No comments:
Post a Comment