MAHAKAMA ya Wilaya ya
Mbeya imewahukumu kifungo cha miaka 120 watu wanne akiwemo aliyekuwa askari wa
jeshi la Polisi baada ya kukutwa na hatia ya unyang’anyi wa kutumia silaha.
Hukumu hiyo imetolewa
na Hakimu wa Mahakama ya Wilaya ya Mbeya, James Mhanusi,ambapo mbali na
kuwatia hatiani washitakiwa hao Mahakama hiyo pia imemuachia huru mshtakiwa
mmoja kwa kile kilichoelezwa kuwa hakuna ushahidi unaomhusisha na tukio moja
kwa moja.
Mwendesha mashtaka wa
Serikali,Catherine Paul, aliwataja washtakiwa kuwa ni aliyekuwa Askari wa Jeshi
la Polisi,8303 Pc James, Elinazi Mshana,Lusajo Jeremia na Abdalah Mohamed ambao
kwa pamoja walitenda kosa la unyang’anyi wa kutumia silaha Oktoba 7, 2013.
Mwendesha mashtaka
huyo alisema watuhumiwa hao wenye kesi namba 23/2014 walitenda kosa hilo
kinyume cha kifungu cha 287 (a) cha kanuni ya adhabu sura ya 16 iliyofanyiwa
marekebisho mwaka 2002 ambapo walifanikiwa kupora Kahawa yenye thamani ya
shilingi Milioni 119.2 yenye uzito wa kilogramu 30091.
Akisoma Hukumu kwa
watuhumiwa hao, Hakimu Mhanusi amesema kutokana na ushahidi wa upande wa
mashtaka na upande wa utetezi mahakama imeona mshtakiwa namba tatu katika kesi
hiyo ambaye ni Gwantwa Malakasuka hakukuwa na ushahidi unaomtia hatiani pasipo
shaka hivyo akaamuru kuachiwa huru.
Kwa upande wa
Washtakiwa wengine, amesema ushahidi wa mazingira pamoja na kutambuliwa na
shahidi wa kwanza ambaye pia ndiye aliyekuwepo eneo la tukio unathibitisha
pasipo shaka kutenda tukio hilo kutokana na kufanya tukio hilo majira ya jioni
wakati kuna mwanga hivyo ilikuwa rahisi kutambuliwa.
No comments:
Post a Comment