KWA MAONI AU USHAURI E-mail: inocomm2014@gmail.com, PIGA SIMU: 0714555668

www.utt-pid.org


TEMBELEA: www.utt-pid.org

January 30, 2015

CHADEMA:VIGOGO WENGI WAMEACHWA ESCROW NAO WASHUGHULIKIWE

Ntagazwa
Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), kimesema sakata la kuchotwa kwa fedha za umma zaidi ya Sh. bilioni 300 kutoka Akaunti ya Tegeta Escrow katika Benki Kuu ya Tanzania (BoT), bado ni bichi iwapo Waziri wa Fedha, Saada Mkuya na Katibu Mkuu wake, Servacius Likwelile na Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT), Prof. Benno Ndulu, hawatahojiwa  na kuwajibishwa.
 
Alisema vigogo hao wanapaswa kuhojiwa kuhusiana na wizi wa fedha hizo kwa kuwa  kutokana na nafasi zao walipaswa kuwa na taarifa wakati fedha hizo zinaondolewa BoT na kwenda katika akaunti za watu walionufaika na mgawo.
 
Pia, kimetaka wahusika wengine wanaodaiwa kuchota kiasi cha Sh. bilioni 160 kati ya bilioni 306 kutoka akaunti hiyo na kuziweka katika Benki ya Stanbic, hivyo kuitaka pia taasisi hiyo ya fedha  kuwaorodhesha wote walioweka fedha hizo huko ili waweze kuchukuliwa hatua kama ilivyokuwa kwa walioweka katika Benki ya Mkombozi.
 
Akizungumza na waandishi wa habari jana jijini Dar es Salaam, Mwenyekiti wa Bodi ya Udhamini ya Chadema, Arcado Ntagazwa, alisema hatua ya kututwa kazi kwa aliyekuwa Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Prof. Anna Tibaijuka na kujiuzulu kwa aliyekuwa Nishati na Madini, Prof. Sospeter Muhongo, haitoshi kufumbua wizi wa fedha hizo za umma katika akaunti. 
 
“Hatua madhubuti za kushughulikia ukwapuaji wa mabilioni ya Shilingi katika akaunti ya Tegeta Escrow hazijakamilika na haziwezi kukamilika bila kuhojiwa au kuwajibishwa kwa Gavana wa Benki Kuu, Prof. Benno Ndulu, Waziri wa Fedha, Saada Mkuya, Katibu Mkuu, Wizara ya Fedha, Dk. Servacius Likwelile,” alisema.
 
Ntagazwa alidai kuwa taifa linaendeshwa kwa ubaguzi na upendeleo huku viongozi wakubwa serikalini wakilindana na kwamba mambo hayo yakiachwa yatazidi kuchochea mbegu za uhasama miongoni mwa jamii na kuliangamiza taifa.

No comments:

Post a Comment