KWA MAONI AU USHAURI E-mail: inocomm2014@gmail.com, PIGA SIMU: 0714555668

www.utt-pid.org


TEMBELEA: www.utt-pid.org

January 23, 2015

NI SHIIDAH:MWENYEKITI NYUMBANI KWA MH.PINDA ALA KICHAPO

i

Uapishaji wenyeviti wa serikali za mitaa katika Manispaa ya Ilala jijini Dar es Salaam kwa mara nyingine umekumbwa na vurugu zilizosababisha aliyekuwa mgombea uenyekiti kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM) kupewa kipigo na wananchi mbele ya askari polisi na kuchaniwa nguo zake kwa madai alitaka kuapishwa kinyemela.
 
Waziri Mkuu, Mizengo Pinda , ametajwa na kulalamikiwa kuwa chanzo cha vurugu hizo kwa kudaiwa kutoa maagizo ya kuapishwa kada kutoka CCM katika mtaa wake bila kushinda uchaguzi.
 
 Aidha,Mwenyekiti wa mtaa wa Migombani kata ya Segerea, Japhet Kembo, hivi karibuni aliapishwa na wananchi kupitia wakili wa kujitegema baada ya uongozi wa manispaa kushindwa kumuapisha kwa wakati, jana aliapishwa rasmi na Mwanasheria wa Manispaa hiyo.
 
Mwingine aliyeapishwa ni Mwenyekiti mteule wa mtaa Minazi mirefu, Ubaya Chuma.
 
 Wakati wa zoezi hilo, Mariano Bungala ambaye aligombea mtaa wa Kigogo Fresh ‘B’ kata ya Pugu, anakoishi Waziri Mkuu, alipewa kichapo na wananchi wakiwamo wafuasi wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kwa madai kuwa hakushinda kwenye uchaguzi wa serikali za mitaa, lakini kwa sababu anatoka mtaa anakoishi Pinda, hivyo ulifanyika ujanja ili aapishwe kinyemela.
 
Vurugu hizo ziliibuka katika ofisi za Manispaa ya Ilala saa saa 3:30 asubuhi muda mfupi baada ya Bungala kuitwa na maofisa wa manispaa ili kuingia ukumbini kuapishwa, lakini alipotaka kuingia tu alidakwa na wananchi na kuanza kupewa kichapo.
 
Vurugu hizo zilisababisha watumishi wa Manispaa hiyo kusitisha kwa muda kazi hiyo katika ofisi zao kushudia vurugu hizo ambazo zilizimwa baada ya polisi kumuokoa Bungala aliyekuwa akiendelea kupewa kipigo.
 
Mgombea wa Chadema katika mtaa huo, Patricia Mwamakula, ambaye alipambana na Bungala katika uchaguzi huo, alisema wakati wa uchaguzi Desemba 14, mwaka jana hakuna mshindi aliyetangazwa baada ya kutokea vurugu.
 
Alisema kutotangazwa kwa matokeo hayo kulifuatia wanachama wa CCM kuchoma masanduku baada ya kubaini kadri kura zilivyokuwa zinaendelea kuhesabiwa ushindi ulikuwa unaelekea kwa mgombea wa upinzani.
 
“Hakuna aliyeshinda kwenye uchaguzi kwenye mtaa wetu, tatizo tunakaa mtaa anaoishi Waziri Mkuu ambaye amesema kuwa hawezi akaongozwa na mwenyekiti anayetoka chama cha upinzani,” alisema.
 
Mwanachama mwingine wa Chadema, Mayama Mkwizu, alisema wananchi wa mtaa wa Kigogo Fresh “B” hawako tayari kuongozwa na mwenyekiti wa CCM ambaye hakushinda kwenye uchaguzi kwa sababu tu ya shinikizo la Waziri Mkuu.
 
“Kura zilipigwa vizuri, lakini CCM walichoma masanduku kabla ya matokeo kutangazwa, kutaka kuapishwa Bungala, ni shinikizo la Waziri Mkuu, kama wanataka kusema alishinda wa CCM walete majivu hapa yaliyotokana na kuchomwa kwa masanduku ya kura au kama Pinda anaona chama chake kimeshinda aje yeye aapishwe,” alisema.
 
Hata hivyo, Bungala akizungumza na waandishi wa habari huku akiwa chini ya ulinzi mkali wa polisi waliokuwa wamemzunguka huku mkono wa shati lake ukiwa umechanwa na kuondolewa kabisa, alisema ana uhakika alishinda uchaguzi huo.
 
KAULI YA BUNGALA
“Nilishinda kwa kupata kura 233 na matokeo yalitangazwa na Afisa Mtendaji Kata ya Pugu ambaye alikuwa msimamizi wa uchaguzi na ndiye aliyeniambie nije niapishwe,” alisema Bungala huku akichechemea kutoka na kipigo alichokipata.
 
Bungala alisema tukio lililompata la kupigwa na ataliwasilisha kwa viongozi wake wa chama na kwamba waliomfanyia vurugu hizo ni wahuni ambao wanataka kuendesha siasa za vurugu.
 
Alipoulizwa kama kuna shinikizo kutoka kwa Waziri Mkuu na kuamua kuja kuapishwa wakati anafahamu kuna utata katika matokeo kwenye mtaa wake, alisema hizo taarifa ni za uongo. 
 
MWANASHERIA WA MANISPAA ANENA
Naye Mwanasheria Mkuu wa Manispaa ya Ilala, Mashauri Musimu, alisema licha ya mwenyekiti wa mtaa Kigogo Fresh “B’ kupigwa na kusababisha asiapishwe, lakini manispaa itahakikisha inafanya kila liwezekanalo aapishwea kwa sababu ndiye mshindi halali katika uchaguzi huo.
 
“Anayetambuliwa na Manispaa kuwa ndiye mshindi ni Mariano Bungala na kama kuna mtu hajaridhika anaruhusiwa kwenda mahakamani kudai haki,” alisema.
 

No comments:

Post a Comment