KWA MAONI AU USHAURI E-mail: inocomm2014@gmail.com, PIGA SIMU: 0714555668

www.utt-pid.org


TEMBELEA: www.utt-pid.org

February 2, 2015

WAGOMBEA URAIS CCM KITANZINI




Mwenyekiti wa CCM, Rais Jakaya Kikwete akiwapungia maelfu ya wananchi wakati akiingia katika uwanja wa Maji Maji mjini Songea mkoani Ruvuma jana, kuongoza kilele cha sherehe za kuadhimisha Miaka 38 ya Kuzaliwa kwa CCM.

MWENYEKITI wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Rais Jakaya Kikwete amewaonya wanachama wa chama hicho, kuheshimu Katiba ya chama na kufuata taratibu katika kugombea nafasi za kuteuliwa katika uchaguzi wa mkuu ili wasije kukilaumu chama, endapo wataenguliwa na hivyo kushindwa kutimiza ndoto zao.
Amesema Katiba na taratibu za chama hicho, zinafahamika hivyo ni muhimu kwa kila mmoja kuziheshimu, ili wasije kukilaumu chama pindi watakapoenguliwa wakati wa mchakato wa kutafuta mgombea wa nafasi mbalimbali kupitia chama hicho.
Rais Kikwete aliyasema hayo jana wakati wa maadhimisho ya Sherehe za Miaka 38 ya Kuzaliwa kwa CCM, zilizofanyika Uwanja vya Majimaji, Songea mkoani Ruvuma, ambapo alisema chama kitateua mgombea ambaye hatakuwa na shaka yoyote kwa wWatanzania.
Aidha, alitaka wanachama kutofanya ajizi katika maslahi ya nchi pamoja na chama kwa ujumla kwa kuteua wagombea wenye sifa katika ngazi zote, watakaoweza kukipa ushindi chama hicho na kuwatumikia wananchi. Akizungumza kwa hisia kali, alisema wapo wanachama wana sifa za kugombea na kuongoza, lakini hawajijui, hivyo alitaka wanachama wenzao wengine kuwashawishi wajitokeze, kwa kuwa suala la kujitokeza sio dhambi kama kukiuka maadili.
“Kama kuna wasiosikika na wapo, tuwashawishi wajitokeze, maana si dhambi kujitokeza, ila ni dhambi kufanya mambo ya kukiuka maadili, tusifanye ajizi katika mambo yenye maslahi kwa taifa,” alisema Rais Kikwete.
Alisema uchaguzi mkuu wa mwaka huu ni wa kihistoria nchini, kwa sababu ni uchaguzi wa kumchagua Rais wa awamu ya tano, huku akipendekeza rais atakayechaguliwa awe ni kutoka CCM na mwenye uwezo wa kuongoza taifa.
Rais Kikwete alisema Watanzania wasikubali kukiuka wosia ulioachwa na Hayati, Mwalimu Julius Nyerere wa kuwa Rais bora atatoka CCM na bila CCM imara nchi itayumba. “Lazima tuhakikishe hatufiki huko, tusikubali kukiuka wosia huu, laana kubwa itatufika na nchi itapata hasara kubwa kwani itayumba kama alivyosema Mwalimu Nyerere,” alisema.
Katiba Inayopendekezwa Akizungumzia Katiba Inayopendekezwa, Rais Kikwete alisema jambo hilo ni kubwa na tayari ameshatoa maagizo kwa ajili ya kuchapishwa kwa nakala za Katiba Inayopendekezwa ili ziweze kusambazwa kwa wingi kwa wananchi waweze kuzisoma.
Aliwataka wanachama na viongozi, kuwashawishi wananchi kujitokeza kuipigia kura ya “Ndiyo” katiba hiyo. Alisema licha ya wapinzani kusema wamejipanga ili katiba hiyo isipite, wananchi wajitokeze kwa wingi na kuipitisha katiba hiyo.
“Katiba Inayopendekezwa imebeba maslahi mapana ya taifa, hatujawahi kuwa na katiba kama hii katika historia ya nchi yetu, katiba hii imekuja na ufumbuzi wa changamoto za Muungano, hivyo hata Zanzibar wataweza kufanya mambo yao kwa uhuru,” alisema.
Rais Kikwete alisema, haoni sababu ya kuikataa Katiba Inayopendekezwa na aliwatahadharisha Watanzania kuwa wakikataa Katiba hiyo, itaendelea kutumika ya sasa. “Mkikataa, hii iliyopo itaendelea kutumika mpaka miaka ijayo, Rais ajaye hatujui kama ni atakayefuata baada ya yangu au baada ya huyo, awe na hamu ya kuanzisha mchakato wa Katiba, mimi nilikuwa na hamu hiyo, sasa atakayekuja anaweza akasema hilo sio kipaumbele chake,” alisema.

No comments:

Post a Comment