KWA MAONI AU USHAURI E-mail: inocomm2014@gmail.com, PIGA SIMU: 0714555668

www.utt-pid.org


TEMBELEA: www.utt-pid.org

June 20, 2015

MTANGAZA NIA URAIS ASHAMBULIWA AKISAKA WADHAMINI.

Dk. Muzzammili Kalokola                                                                                                                         
Kada wa CCM aliyetangaza nia ya kugombea urais kupitia chama hicho wiki iliyopita, Dk. Muzzammili Kalokola,  juzi alijionja joto ya jiwe baada ya kupata kipigo kutoka kwa vijana wa ulinzi wa Green Guard wakati akisaka wadhamini mkoani Tanga.


Akisimulia mkasa huo kwa mwandishi wa NIPASHE kwa njia ya simu jana, alisema , Jumatano baada ya kuwasili nje za ofisi hizo kama alivyotakiwa na Katibu wa wilaya hiyo, ghafla alivamiwa na kundi la Green Guard wakimtaka aondoke.


Alisema walimshambulia kwa kumpiga kisha kumkata mtama na kudondoka, huku Katibu Mwenezi wa Wilaya, akitamka aondolewe katika eneo hilo kwa madai kuwa ‘Mkutano hauwezi kuandaliwa na mwingine halafu mtu mwingine azungumze’.


Tukio la shambulio hilo pia limeonyeshwa katika mitandao mbali mbali ya kijamii, ambapo mtangaza nia huyo alionekana akipigwa na kundi hilo na kuondolewa.


Alisema katibu huyo aliwaeleza vijana hao wamwondoe lakini akiwa eneo hilo la tukio alimpigia simu katibu wa wilaya aliyemtaka awali afike hapo saa 6:00 mchana kuomba udhamini.


“Wakati Katibu wilaya akija eneo la tukio, niliwasiliana pia na Kamanda wa Polisi mkoa wa Tanga (RPC) ambaye awali nilipeleka malalamiko yangu kwake dhidi ya hujuma ninazofanyiwa,” alisema.


Alisema baada ya katibu wa wilaya kufika alimpa simu na kuzungumza na RPC na baadaye alilazimika kwenda polisi na kupewa RB/Tan/58000/2015.


 “Kada mwenzangu ndiye anayenichafua, maana nimefika hapa nikavamiwa ghafla halafu jioni saa 12:00 huyo kada alikuja kuomba ridhaa ya wadhamini,” alisema.


Akielezea hujuma alizofanyiwa, Dk. Kalokola alisema baada ya kuchukua fomu Dodoma alipewa barua za utambulisho kwa kila katibu wa mkoa ili wakasaini daftari la wageni na hatua nyingine zifuate.


Alisema mwanzoni mwa wiki hii alienda ofisi ya katibu wa wilaya Tanga, ambapo huko alimkuta kaimu wake ambaye alimweleza kuwa, ofisi inamtayarishia mtangaza nia Bernald Membe na Amina Salum Ali.


Alisema baada ya maelezo hayo, kesho yake alimwandikia barua Katibu Mkuu wa chama Dodoma kwa sababu barua alizopewa zinaeleza wazi kuwa, kila mtangaza nia atendewe haki.


Alisema siku hiyo wakati akijiandaa kwenda kwa RPC wa Tanga, ofisi ya wilaya iliwatuma watu wakamwite.


“Niliwajulisha kuwa nitaenda baadaye kwa sababu nilikuwa naenda polisi, baadaye nilipoenda katibu wa wilaya sikumkuta nilirudi kesho yake asubuhi nikaambiwa kesho yake niende kwa ajili ya kukutana na wadhamini,” alisema na kuongeza:

“Kwa kuwa Alhamisi nilitakiwa kwenda Dar es Salaam kwenye kesi ya katiba, nilimuomba ifanyike siku hiyo ya Jumatano, alikubali na kunitaka saa 6:00 mchana nirudi ofisi hapo,” alisema.


Alisema muda ulipofika alienda ndipo alipoambulia kipigo hicho.CHANZO:NIPASHE

No comments:

Post a Comment