KWA MAONI AU USHAURI E-mail: inocomm2014@gmail.com, PIGA SIMU: 0714555668

www.utt-pid.org


TEMBELEA: www.utt-pid.org

June 17, 2015

SERIKALI KUFANYIA KAZI WAZO LA ‘TFF’ MOJA

SERIKALI imeahidi kukaa pamoja na vyama vya soka vya Tanzania (TFF) na Zanzibar (ZFA) ili kuona uwezekano wa kuwa na chama kimoja kitakachoendesha mchezo huo sehemu zote za Muungano.

Ahadi hiyo ilitolewa bungeni jana na Naibu Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, Juma Nkamia wakati akijibu swali la nyongeza la Mbunge wa Tabora Mjini, Ismail Aden Rage (CCM) aliyehoji uwezekano wa kuunganisha vyama hivyo vya mpira kama ilivyo kwa Kamati ya Olimpiki (TOC) ambayo sasa inaongozwa na Mzanzibari.

“Kuwa na chama kimoja kama ilivyo TOC ni lazima tushirikishe wadau wote, tukae pamoja na kuongea ili kusitokee malumbano. Ni wazo zuri, tumelipokea na tutalifanyia kazi,” alisema Nkamia.

Kadhalika, Nkamia alisema TFF muda wote imekuwa ikiunga mkono juhudi zozote zinazofanywa na ZFA za kuwa mwanachama mshiriki wa Shirikisho la Soka Duniani (FIFA) kama zilivyo ‘nchi’ zisizo na mamlaka kamili za Hong Kong na Macau.

TFF pia imekuwa ikiunga mkono juhudi za ZFA kuwa mwanachama mshiriki wa Shirikisho la Soka la Afrika.
Nkamia aliyasema hayo akijibu swali lingine la nyongeza la Mbunge wa Kilwa Kaskazini, Murtaza Mangungu (CCM) aliyetaka kujua endapo kuna namna yoyote ambayo TFF inaweza kuisaidia ZFA kuwa mwanachama wa Fifa.

Mapema, Mbunge wa Kikwajuni, Hamad Yussuf Masauni (CCM), aliuliza kama inawezekana kuwa na mashirikisho matatu nchini, yaani mbali na ZFA na TFF kuwe na lingine litakalofanya kazi sehemu zote za muungano “ili Wazanzibari nao wanufaike na misaada inayotolewa na Fifa.

Akijibu, Nkamia alisema hilo linaweza kuwa gumu kutokana na muundo wa muungano wa nchi yetu wa serikali mbili.

Katika swali la msingi, Mbunge wa Baraza la Wawakilishi, Jako Hashim Ayoub alitaka kujua kwa nini uongozi wa sasa wa TFF ulikwenda Zanzibar na kuidanganya ZFA kwamba utaipigania ipate uanachama Fifa wakati ukijua haiwezekani kwa kuwa Fifa ilishasema Zanzibar haiwezi kupata uanachama katika mfumo wa Muungano.

Akijibu swali hilo, Nkamia alisema wizara yake haina taarifa juu ya ahadi iliyotolewa na TFF kwamba ‘itahakikisha’ Zanzibar inapata uanachama Fifa, bali kinachosisitizwa na TFF ni kuunga mkono juhudi zozote endapo kutatokea mabadiliko katika taratibu za Fifa na hivyo kufungua milango kwa ZFA kupata uanachama. (HABARI LEO)

No comments:

Post a Comment