Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru),
inatarajia kuanza kuwasaka viongozi wa umma waliotumia nafasi zao vibaya
ikiwamo kuiba na kujilimbikizia mali ndani na nje ya nchi.
Viongozi hao watasakwa na Takukuru kupitia kitengo maalum
kilichoanzishwa mwaka jana ambacho kimeanza kupewa mafunzo nchini Uingereza.
Mkurugenzi Mkuu wa Takukuru, Dk. Edward Hoseah (pichani), aliyasema hayo jijini
Dar es Salaam juzi alipokuwa akijibu baadhi ya maswali ya waandishi wa habari.
Dk. Hoseah aliyasema hayo muda mfupi baada ya kufungua
mafunzo ya watumishi wa Takukuru ambao wapo katika kitengo hicho ili kuwajengea
mbinu na uwezo wa kufanya uchunguzi dhidi ya viongozi walioiba na
kujilimbikizia mali.
Alisema kitengo hicho
cha Takukuru pia kitakuwa na kazi ya kupambana na masuala ya utakatishaji wa
fedha haramu kwa kuwa tatizo hilo linazidi kukua hapa nchini.
Aliongeza kuwa kitengo hicho kilianzishwa rasmi mwaka jana,
lakini hakikuanza kazi yake kutokana na kuchelewa kupatikana mtalaam wa kutoa
mafunzo kwa watumishi hao.
''Tumejizatiti kukabiliana na viongozi wa umma
waliojilimbikizia mali kwa kutumia watalaam wetu ambao wanapatiwa
mafunzo," alisema.
Dk. Hoseah alisema huu ni mwanzo na kwamba watahakikisha
wanafanya kazi vizuri ili kuwabaini watu walioiba na kujilimbilikizia mali huku
akisema kwamba sheria ni msemeno .
Kuhusu wanasiasa wanaodaiwa kujihusisha na vitendo vya
rushwa hususan katika kipindi hiki cha kuelekea uchaguzi mkuu, Dk. Hoseah
alisema mtu yeyote asithubutu kufanya hivyo kwa kuwa Takukuru imesambaa kila
wilaya na kwamba watakamatwa.
''Hawa wagombea
wasifanye mchezo mchafu, ninawaonya kwa kuwa tutawakamata popote walipo,"
alisisitiza. Aliwaonya wanasiasa wanapita maeneo mbalimbali na kuanza kuchonga
barabara na kutoa zawadi nyingine kwa kuwa kufanya hivyo ni kosa na Takukuru
itawashughulikia.
Aliongeza kuwa mtu yeyote atakayepindisha sheria kwamba
Takukuru ipo macho muda wote na itawamulika wanasiasa ama wapambe wao ambao
watataka kuwahonga wananchi kuwashawishi wawapigie kura.
Hata hivyo, kauli ya Dk. Hoseah imekuwa ya kawaida kutolewa
kwa kuwa aliwahi kutangaza vita na wala rushwa wakubwa hapa nchini huku
akiahidi kuwaburuza mahakamani, lakini mpaka leo hakufanya hivyo.
|
July 31, 2015
TAKUKURU KUWASHUKIA VIONGOZI WALIOJILIMBIKIZIA MALI NJE YA NCHI
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment