Lowassa |
Wakati
joto la uchujaji wa majina ya wagombea urais kupitia Chama Cha
Mapinduzi (CCM) likizidi kuongezeka, taarifa zimezidi kuzagaa mitaani na
kwenye mitandao ya kijamii kwamba, mikakati ya kumuondoa Edward Lowassa
kwenye orodha ya watia nia nayo imezidi kupamba moto.
Kwa muda sasa NIPASHE imekutana na makundi mbalimbali ya wasaka
urais na ajenda kuu inayozungumzwa ni mizengwe ya kumwengua Lowassa
kwenye kinyang’anyiro hicho ili kuwarahisishia wengine njia ya kuteuliwa
na chama kwa kuwa anaonekana kuwa kikwazo kwa baadhi ya washindani
wake.
Ofisa mmoja wa CCM makao makuu mjini hapa, aliiambia NIPASHE kuwa
wanachofanya wao kama watendaji ni kuandaa majina ya wagombea wote na
fomu zao za udhamini na kisha kukabidhi kwa sekretarieti itakayopanga
ajenda za vikao vya Kamati Kuu na baadaye Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC)
ya taifa.
Ofisa huyo alipoulizwa kama ana taarifa za kuwako kwa mizengwe
dhidi ya Lowassa alisema kwa ujumla kwa sasa kuna maneno mengi sana
yanazungumzwa juu ya mchakato wa uteuzi wa mgombea, ila akasisitiza kuwa
la msingi ni kusubiri vikao vya maamuzi.
“Ndugu yangu ukiyatazama haya makundi (ya urais) ni vigumu kuamini
kama wanatoka chama kimoja. Yaani kuna kukamiana kweli kweli.
Kila mmoja anataka kumwangusha mwenzake ili yeye apite,” alisema na kuongeza kuwa:
“Hata kama kuna mizengwe, si unajua uchaguzi huu ni wa vyama vingi.
CCM haishindani pekee yake, kwa hiyo mgombea anayekubalika ndiye
anatakiwa.”
Hata hivyo, kwa muda sasa kumekuwa na mfululizo wa habari za
kupikwa kwamba jina la Lowassa litaishia Kamati Kuu kwa madai kwamba
kuna ushahidi wa matumizi ya fedha kwa timu yake, tuhuma ambazo binafsi
(Lowassa) amezikanusha mara kadhaa. Julai mosi mwaka huu siku anarejesha
fomu za kuwania urais kupitia CCM alitoa changamoto kwa yeyote mwenye
ushahidi wa kuhusika kwake na rushwa ajitokeza na kusema alitoa lini,
wapi na kwa nani.
Akizungumza na mamia ya wanachama wa CCM makao makuu Dodoma siku
hiyo, mbali ya kuwashukuru wote waliomdhamini, Lowassa alisema amechoka
kwa tuhuma za kipuuzi za kuhusishwa na rushwa na kusisitiza kuwa hakuna
mwanachama yeyote miongoni mwa zaidi ya nane waliomdhamini aliyefanya
hivyo kwa kishawishi cha fedha au fadhila yoyote.
NIPASHE imedokezwa kwamba miongoni mwa mikakati inayosukwa
kumwangamiza Lowassa ni pamoja na kutengenezwa kwa taarifa za
mawasiliano ya siku kuonyesha kwamba kuna fedha nyingi zimetumwa kwa
wanachama wa CCM ili kuwashawishi kumuunga mkono.
Mgombea anayetajwa kutumiwa zaidi na kundi linalompinga Lowassa ni
pamoja na Makongoro Nyerere, ambaye alifanya mkutano na waandishi wa
habari hivi karibuni na kuporomosha kauli kali za ukakasi dhidi ya
Lowassa.
Wakati mizengwe ikizidi kusukwa dhidi ya Lowassa, ripoti ya kura
zote za maoni ambazo zimekuwa zikitolewa katika miezi ya hivi karibuni
zimeonyesha kuwa Lowassa anaongoza kwa mbali kama chaguo la wananchi
wengi kwenye nafasi hiyo.
Miongoni mwa tafiti hizo ni ule wa Mpango wa Utafiti na Elimu ya
Demokrasia (REDET) ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, uliofanywa mwezi
uliopita na matokeo yake kutolewa mwishoni mwa wiki unaonyesha kuwa
Lowassa ni changuo la kwanza la wengi kwa kujipatia asilimia 27.0 ndani
ya chama hicho, huku Bernard Membe akishikilia nafasi ya pili kwa kupata
asilimia 8.2.
Katika utafiti huo ambao REDET walisema kuwa unaweza kuchukuliwa
kwa ujumla wake kama maoni ya Watanzania endapo masuala yaliyoulizwa
uchaguzi ungefanyika katika kipindi cha utafiti, wahojiwa walikuwa 1,250
kutoka wilaya moja moja katika mikoa 25 ya Tanzania Bara.
Wakati mkakati wa mizengwe ukiendelea kupamba moto, wajumbe wa
sekretarieti ya Kamati Kuu ya chama hicho wanaanza vikao mjini hapa leo
kundaa pamoja na mambo mengine ajenda na taarifa kwenye vikao vya Kamati
Kuu itakayokaa Alhamisi mjini hapa.
Kikao cha Kamati Kuu kinatarajiwa kuchuka majina ya watia nia 38
waliojitokeza kutafuta ridhaa ya chama hicho na kubakisha majina matano
tu yatakayopelekwa NEC kwa kupigiwa kura.
NEC inayotarajiwa kukutana Ijumaa wiki hii, itatoa majina matatu
kwenda Mkutano Mkuu unaotarajiwa kukutana Jumamosi kwa ajili ya kupata
jina moja la mgombea urais wa CCM katika uchaguzi mkuu wa Oktoba 25,
mwaka huu.
CHANZO:
NIPASHE
No comments:
Post a Comment