KWA MAONI AU USHAURI E-mail: inocomm2014@gmail.com, PIGA SIMU: 0714555668

www.utt-pid.org


TEMBELEA: www.utt-pid.org

September 22, 2015

LOWASSA: NITAUNDA TUME YA MIKATABA YA GESI ASILIA

Mgombea Urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Chadema, Edward Lowassa akihutubia umati wa wananchi katika kampeni zake zinazoendelea.
Mgombea Urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Chadema, Edward Lowassa akihutubia umati wa wananchi katika kampeni zake zinazoendelea.
MGOMBEA urais kwa tiketi ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), anayeungwa mkono na vyama vya upinzani vinavyounda Ukawa, Edward Lowassa amewaahidi wakazi wa Mtwara kuwa endapo atachaguliwa kuwa rais, ataunda tume maalumu kuchunguza mikataba ya gesi asilia.

Lowassa alisema kuwa kwa kuwa gesi sasa imeshatoka kwenda Dar es Salaam, si wakati tena wa kupinga isitoke, lakini ipo haja kwa serikali yake atakayoiunda, kuchunguza mikataba yote ya gesi ili kujiridhisha kama haikuingia kwa hila. “Ndugu zangu wa Mtwara gesi inatoka, haitokiiiiii?....inatokaaaaaaa?.

Ngoja niwaambieni hivi, mkinichagua kuwa rais nitaunda tume maalumu ambayo itachunguza mikataba yote ya gesi ili kujiridhisha kama ilikuwa sahihi au hapana ;na watakaohusika tutawafikisha katika vyombo vya sheria, washughulikiwe kwa mujibu wa sheria,” alisema Lowassa.

Lowassa aliyasema hayo baada ya mamia ya watu wakazi wa Mtwara, waliofika katika mkutano wake kumsikiliza kumhoji kwa nini hazungumzii suala la gesi. Walifanya hivyo baada ya Lowassa kuonekana kumaliza hotuba yake, bila kulitaja suala hilo, ambalo wakazi wa Mtwara wanadai ni ajenda yao.

“Nadhani tumeelewana, eti upande ule kule mmenielewa suala hili la gesi? Nataka tulimalize kwa namna hii, sawaa?...lazima tuwashughulikie waliohusika kama vyombo vitawaona wana hatia”, alisema Lowassa.
Awali, mgombea huyo aliwaahidi wakazi wa Mtwara kuwa serikali atakayoiunda, itakuwa makini na itahakikisha hakuna hata mtanzania mmoja, atakayekuwa masikini katika kipindi kifupi cha uongozi wake.

“Nachukia umasikini, ndio maana nimegombea nafasi hii...nataka kwa aliye na baiskeli moja, anunue ya pili ;na kama unakula mlo mmoja ule milo mitatu ;na aliye na mke mmoja aoe wa pili kama dini yake inamruhusu,” alisema Lowassa.

Alisema atatengeneza mazingira mazuri kwa mamantilie, bodaboda na wamachinga ili wafanye kazi zao kwa tija. Akimkaribisha Lowassa kuzungumza na wananchi, Waziri Mkuu mstaafu Frederick Sumaye alisema kuwa CCM imeshindwa kuwaletea maendeleo wananchi kwa haraka; na inapaswa kuondoka madarakani kumpisha Lowassa, alete maendeleo kwa haraka. 

Kabla ya kufanya mkutano wake mjini Mtwara katika viwanja vya Mashujaa, Lowassa alihutubia mikutano miwili katika wilaya za Newala na Tandahimba.

No comments:

Post a Comment