Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Amos Makalla amekumbana na joto la Mbeya baada ya
 meya wa jiji hilo, Mchungaji David Mwashilindi na madiwani wake 34 
kususia kikao chake cha kujitambulisha kwa wananchi, baada ya kudaiwa 
kwenda kukagua Soko la Mwanjelwa bila kumpa taarifa yoyote meya wa jiji 
hilo. 
Meya alifikia uamuzi huo ndani ya ukumbi wa Mkapa muda 
mfupi kabla ya Makalla kuanza kuzungumza na watumishi wa jiji, wananchi,
 wazee maarufu, viongozi wa dini na machifu ambapo Mkuu wa Wilaya ya 
Mbeya Nyirembe Sabi alimkaribisha Meya Mwashilindi kuzungumza chochote 
kwa niaba ya madiwani wake. 
Hata hivyo, Meya Mwashilindi 
alipochukua kipaza sauti alisema: “Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, nakumbuka kwa 
mara ya kwanza kukutana na wewe tulizungumza kwamba tufanye kazi, siasa 
zimekwisha. Lakini masikitiko yangu ni kwamba leo hii umekwenda Soko la 
Mwanjelwa bila ya mimi mwenye jiji kupewa taarifa yoyote wala madiwani 
wangu. Sasa hiki kikao hakinihusu hivyo muendelee na kikao chenu.” 
Baada
 ya kusema maneno hayo alikabidhi kipaza sauti kwa mkuu wa wilaya, kisha
 akachukua nyaraka zake akainuka pamoja na madiwani wote kupitia Chadema
 na kutoka ukumbini huku wakisikika wakisema, ‘hizi ni siasa ambazo 
tulizikataa, lakini wanatulazimisha kuendesha siasa. Hatuwezi kupuuzwa 
kwa kiasi hiki.” 
Mkuu wa Wilaya, Mnasa alisema anaamini taratibu
 na ratiba yote ilipangwa vizuri hivyo hawaoni sababu ya madai ya 
madiwani hao kwamba hawakushirikishwa kwenye ziara hiyo, wao kama 
wawakilishi wa Rais hawaangalii siasa, bali wanaangalia uchapakazi na 
siyo masuala ya siasa. 
Akizungumzia kitendo cha meya na madiwani
 wake kususia kikao hicho, Makalla alisema ‘Nashangazwa na uamuzi wa 
madiwani hawa kwa kitendo hiki, kwani siku ile nilipotembelea Shule ya 
Sekondari Iyunga, nilisema kwamba Aprili 20 ambayo ndiyo leo (jana) 
nitakuwa na ziara ya jiji na kabla ya kikao nitataka kutembelea Soko la 
Mwanjelwa,” alisema Makalla. 
Alisema suala la meya na madiwani 
wake kutoshirikishwa kwenye ziara ya kwenda Soko la Mwanjelwa halimhusu,
 kwani mwenye wajibu wa kupeana taarifa ni kwenye ngazi ya halmashauri 
ya jiji, lakini siyo yeye (Makalla). 
“Jamani mimi sijaja kufanya
 siasa nimekuja kufanya kazi ya wananchi na nilishatahadharisha jambo 
hili, sasa kwa kitendo hiki ndiyo siasa na wananilazimisha kufanya 
siasa, lakini wao ndiyo watahukumiwa na wananchi. Na ninasema kama Mola 
ataendelea kunilinda kubaki katika mkoa mwaka 2020 nitakwenda kuwaambia 
hiki kinachofanyika sasa na wawakilishi wao,” alisema Makalla.
Awali 
Makalla akiwa katika Soko la Mwanjelwa alinusa harufu ya ufisadi kwenye 
soko hilo na kuagiza vyombo vya ulinzi na usalama mkoa huo, kufanya 
uchunguzi ndani ya wiki nne wa uhalali wa fedha kiasi cha Sh22.9 bilioni
 iliyotumika katika ujenzi huo ukiwa ni mkopo kutoka Benki ya CRDB. 
Makalla
 alitoa agizo hilo jana mchana baada ya kutembelea soko hilo na 
kuzungumza na wafanyabiashara wa jijini hapa, ambao walimueleza 
wanashindwa kumudu gharama ya upangaji ya vyumba vya biashara ambayo 
inaanzia kiasi cha Sh500,000 kwa chumba kimoja kwa mwezi, ndiyo maana 
hawataki kuingia ndani ya soko hilo. 
Mwenyekiti wa soko hilo, 
Peter Chacha alimueleza Makalla kwamba wasipokuwa makini soko hilo 
litabaki gofu, kwani wafanyabiashara hawataki kuingia kwa kuogopa 
gharama kubwa ya vyumba hivyo, alimuomba afanye awezalo kukaa chini na 
uongozi wa benki ambao unadai fedha zao kwa jiji na kuona namna ya 
kupunguziwa gharama hiyo. 
“Ni kweli wenzetu jiji, wametingwa na 
deni la mkopo kutoka Benki ya CRDB, ndiyo maana wamekuja kutubana sisi 
wafanyabiashara kwa kutupangia chumba kuanzia Sh500, 000 hadi Sh 
800,000, kitu ambacho hatuwezi kumudu hata kidogo,”alisema 
Chacha 
Baada ya kusikiliza kilio cha wafanyabiashara hao, Makalla 
alisema kiasi cha Sh22.9 bilioni iliyotumika kwenye ujenzi wa soko hilo 
haiendani na thamani yake, hivyo vyombo vya dola vikiongozwa na Kamanda 
wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) Mkoa wa Mbeya, 
wanafanya uchunguzi wa kina na kuwanasaka wale wote waliohusika kwenye 
mchakato mzima wa ujenzi wa soko hilo. 
“Nataka kupata taarifa ya
 mchanganuo mzima wa namna ya fedha ilivyokopwa, ilivyotumika na mkataba
 wake ulivyokuwa ndani ya wiki nne, taarifa hii niipokee na wale 
watakaobainisha kufuja fedha watapelekwa mahakamani kwa mujibu wa 
sheria. 
"Kwenye hili, kuna watu waliotufikisha hapa, Sh22.9 
bilioni iliyotumika kwenye ujenzi huu haiendani na ujenzi wa soko hili, 
kuanzia muda uliotumika na gharama ya kodi ya upangishaji wa vyumba siyo
 rafiki ni kubwa mno, hivyo jiji na CRDB mkae muone namna ya kupunguza 
gharama hiyo, kwani hali ilivyo sasa lile soko litabaki gofu."
 



 
No comments:
Post a Comment