KWA MAONI AU USHAURI E-mail: inocomm2014@gmail.com, PIGA SIMU: 0714555668

www.utt-pid.org


TEMBELEA: www.utt-pid.org

August 16, 2016

DANGOTE, MENGI WAIGOMBEA YANGA


ZAITUNI KIBWANA NA ZAINAB IDDY
BILIONEA maarufu Afrika, Mnigeria Aliko Dangote, amejikuta akiwa vitani na mfanyabiashara maarufu hapa nchini ambaye ni Mwenyekiti wa Makampuni ya IPP, Reginald Mengi, katika suala zima la kuimiliki klabu ya soka ya Yanga.
Wawili hao wamejikuta wakiwa na nafasi kubwa ya kufanikisha azma yao hiyo baada ya bilionea aliyekuwa akiibeba Yanga kwa muda mrefu, kuamua kuachia ngazi.
Habari zilizozagaa kwenye mitandao Dar es Salaam jana na kuthibitishwa na mmoja wa wanachama maarufu wa klabu hiyo, Jerry Muro, zinasema kuwa bosi huyo amefikia uamuzi huo ikiwamo kujiuzulu nafasi yake ya uongozi kutokana na kile alichosisitiza ‘imetosha’.
Na habari zaidi zinadai kuwa Mengi ameonyesha nia kitendo kilichowafanya baadhi ya wanachama wa klabu hiyo wakiwamo wazee wao, kupanga kumfuata kumtaka afanye hivyo.
Na iwapo Mengi atakubali, ni wazi atakuwa na kazi kubwa ya kushindana na Dangote aliyezaliwa Aprili 10, 1957 anayemiliki Kampuni ya Dangote Group, inayoendesha biashara zake katika nchi mbalimbali za Afrika zikiwamo Benin, Ethiopia, Senegal, Cameroon, Ghana, Afrika Kusini, Togo, Tanzania na Zambia.
Mnigeria huyo anatajwa kuwa na utajiri wa Dola za Marekani bilioni 14.9 sawa na Sh trilioni 32.5, akitajwa kushika nafasi ya 67 katika orodha ya matajiri duniani, huku akiwa wa kwanza Afrika.
Na iwapo mmoja wa wawili hao atafanikiwa kuitwaa Yanga, ni wazi kuwa klabu hiyo itakuwa haijapoteza chochote baada ya kujiuzulu kwa bilionea wao.
Juu ya kujiuzulu kwa bosi huyo wa Yanga, imedaiwa kuwa kumetokana na kuchoshwa na shutuma zinazotolewa na baadhi ya viongozi wa Serikali na wengine kutoka ndani ya klabu hiyo ambao wanatumiwa na baadhi ya wafanyabiashara kwa masilahi yao binafsi.
Mbali na taarifa hizo, chanzo cha ndani ya Yanga, kimeliambia BINGWA kuwa kiongozi huyo mara kwa mara amekuwa akiumizwa na tabia za baadhi ya watu ndani ya timu hiyo hususani wanachama kumtukana na kumkebehi kwa hatua yake ya kutaka kuimiliki timu.
“Suala la kujiuzulu ni kweli na hii inatokana na baadhi yetu wanachama kufanya mambo anayoona kama anadharauliwa na kudhihakiwa, hivyo ameona bora akae pembeni ili kulinda heshima yake.
“Tangu jambo hilo kuibuka mchana huu (jana), viongozi wa Yanga wamekuwa wakihaha kufanya mawasiliano naye, lakini pia wakipishana katika ofisi yake ili kumsihi asitangaze uamuzi huo,” alisema.
Chanzo chetu hicho kilizidi kupasha: “Tayari wazee wameshakubaliana leo (jana) jioni kukaa na Mengi ili kuona jinsi watakavyoweza kuisaidia Yanga mara tu bilionea wao atakapotangaza rasmi uamuzi wake huo.”
BINGWA lilimtafuta Kaimu Katibu Mkuu wa Yanga, Baraka Deusdedit, ambapo alisema taarifa hizo amezisikia, lakini hawezi kuzungumzia hadi awe na uhakika juu ya jambo hilo.
“Hizi taarifa na mimi nimezisikia pia, lakini siwezi kuzungumzia lolote kwani sijapata taarifa maalumu juu ya jambo hilo, zinaweza kuwa kweli au si kweli,” alisema.
Ujio wa Dangote au Mengi ndani ya Yanga, utaifanya klabu hiyo kuendelea kuwa tishio nchini na Afrika kwani haitakuwa na shida kama ilivyokuwa kwa kipindi chote chini ya bilionea wao aliyedaiwa kutangaza kujiondoa Jangwani jana.
Katika hatua nyingine, wanachama na mashabiki wa Yanga jana walifurika makao makuu ya klabu hiyo katika kile kinachoonekana kutokubaliana na mpango wa kujiuzulu kwa bilionea wao huyo.
BINGWA lilifika katika jengo lao lililopo makutano ya Mtaa wa Twiga na Jangwani, Dar es Salaam na kukuta umati wa mashabiki wa Yanga waliokuwa wakiwashutumu baadhi ya viongozi wao kwa kile walichodai wao kuwa sababu ya kujiuzulu kwa ‘mfalme’ wao huyo ambapo waliwaonya kufanya kile kinachowezekana kuinusuru klabu yao.Chanzo Bingwa.

No comments:

Post a Comment