KWA MAONI AU USHAURI E-mail: inocomm2014@gmail.com, PIGA SIMU: 0714555668

www.utt-pid.org


TEMBELEA: www.utt-pid.org

August 24, 2016

MAJALIWA: ONDOENI WATU WALIOVAMIA MAENEO YALIYOHIFADHIWA

MAJI
 Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa na Mkewe Mary wakitazama ngoma ya asili ya Wapimbwe wakati walipowasili kwenye uwanja wa kijiji cha Majimoto wilayani Mlele kuhutubia mkutano wa hadhara Agosti 23, 2016. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)
MAJI1
 Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akikagua ujenzi wa daraja la mto Kavuu wilayani Mlele Agosti 23, 2016. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)
………………………………………………………………..
WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa ameuagiza uongozi wa wilaya ya Tanganyika mkoani Katavi kuhakikisha unawaondoa watu wote wanaoishi katika maeneo ya hifadhi na ushoroba  wa wanyama  wa Lyamgoroka.
Agizo hilo limetolewa jana jioni (Jumatatu, Agosti 22, 2016) na Waziri Mkuu  wakati akizungumza na wananchi kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika katika kiwanja cha  Majalila wilayani Tanganyika.                    
Waziri Mkuu alisema wilaya hiyo inatakiwa kuendelea kuwaondoa watu wote waliovamia na kujenga makazi  ndani ya Hifadhi ya Taifa ya Katavi  ili kuepuka uharibifu wa mazingira.
“Hakikisheni mnatunza mazingira. Msiache wakate miti hovyo kwa sababu wanakausha vyanzo vya maji na kusababisha eneo kuwa hatarini kukumbwa na ukame, hivyo ni vyema wakaondolewa mapema,” alisema.
Katika hatua nyingine Waziri Mkuu amewataka Maofisa Ushirika na Kilimo katika mkoa wa Katavi kuwasaidia wakulima wa tumbaku kwa kuhakikisha wanapata soko la uhakika na kulipwa kwa wakati.
Waziri Mkuu alitoa agizo hilo baada ya kupokea malalamiko ya wananchi kupitia mabango waliyokuwa wameyabeba ambayo yalikuwa yakiwalalamikia maofisa hao kwa kushindwa kuwatafutia masoko na  badala yake wanawakumbatia wabadhilifu wa fedha za ushirika.
“Hatuwezi kuwa na Ofisa Kilimo ambaye hajui masoko ya mazao ya wakulima wake.Mnakaa ofisini tu! Hamfanyi kazi. Lazima mfuatilie masuala ya kilimo katika maeneo yenu, sasa chukua mabango yote yanayohusu zao la tumbaku na ukalete majibu kwa wakulima,” alisema.
Awali Waziri Mkuu alitembelea eneo lililotengwa kwa ajili ya ujenzi wa ofisi za halmashauri na wilaya Tanganyika ambapo aliwapongeza wakazi wa kijiji cha Majalila kwa kutoa bure ardhi yenye ukubwa wa ekari 500 ili Serikali iweze kujenga ofisi hizo.

No comments:

Post a Comment