Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa na
Mkewe Mary wakitazama ngoma ya asili ya Wapimbwe wakati walipowasili
kwenye uwanja wa kijiji cha Majimoto wilayani Mlele kuhutubia mkutano wa
hadhara Agosti 23, 2016. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)
Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa
akikagua ujenzi wa daraja la mto Kavuu wilayani Mlele Agosti 23, 2016.
(Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)
………………………………………………………………..
WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa
ameuagiza uongozi wa wilaya ya Tanganyika mkoani Katavi kuhakikisha
unawaondoa watu wote wanaoishi katika maeneo ya hifadhi na ushoroba wa
wanyama wa Lyamgoroka.
Agizo hilo limetolewa jana jioni
(Jumatatu, Agosti 22, 2016) na Waziri Mkuu wakati akizungumza na
wananchi kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika katika kiwanja cha
Majalila wilayani Tanganyika.
Waziri Mkuu alisema wilaya hiyo
inatakiwa kuendelea kuwaondoa watu wote waliovamia na kujenga makazi
ndani ya Hifadhi ya Taifa ya Katavi ili kuepuka uharibifu wa
mazingira.
“Hakikisheni mnatunza mazingira.
Msiache wakate miti hovyo kwa sababu wanakausha vyanzo vya maji na
kusababisha eneo kuwa hatarini kukumbwa na ukame, hivyo ni vyema
wakaondolewa mapema,” alisema.
Katika hatua nyingine Waziri Mkuu
amewataka Maofisa Ushirika na Kilimo katika mkoa wa Katavi kuwasaidia
wakulima wa tumbaku kwa kuhakikisha wanapata soko la uhakika na kulipwa
kwa wakati.
Waziri Mkuu alitoa agizo hilo
baada ya kupokea malalamiko ya wananchi kupitia mabango waliyokuwa
wameyabeba ambayo yalikuwa yakiwalalamikia maofisa hao kwa kushindwa
kuwatafutia masoko na badala yake wanawakumbatia wabadhilifu wa fedha
za ushirika.
“Hatuwezi kuwa na Ofisa Kilimo
ambaye hajui masoko ya mazao ya wakulima wake.Mnakaa ofisini tu!
Hamfanyi kazi. Lazima mfuatilie masuala ya kilimo katika maeneo yenu,
sasa chukua mabango yote yanayohusu zao la tumbaku na ukalete majibu kwa
wakulima,” alisema.
Awali Waziri Mkuu alitembelea eneo
lililotengwa kwa ajili ya ujenzi wa ofisi za halmashauri na wilaya
Tanganyika ambapo aliwapongeza wakazi wa kijiji cha Majalila kwa kutoa
bure ardhi yenye ukubwa wa ekari 500 ili Serikali iweze kujenga ofisi
hizo.
No comments:
Post a Comment