Azam FC
UJIO
wa makocha kutoka Hispania ndani ya Azam FC, umeanza kuitangaza timu
hiyo kutokana na watu wengi wa nchi hiyo kuanza kuwafuatilia mabingwa
hao wa Klabu Bingwa Afrika Mashariki na Kati.
Uongozi wa Azam FC kabla ya kuanza msimu huu, iliwaajiri makocha
kutoka nchini hiyo inayosifika kuwa na Ligi Kuu bora duniani 'La Liga
Santander' ikijitambulisha kwa soka lake la pasi na mchezo wa kasi.
Joto hilo la makocha linaundwa na Kocha Mkuu, Zeben Hernandez,
Msaidizi wake, Yeray Romero, Kocha wa Viungo, Pablo Borges, Kocha wa
Makipa, Jose Garcia na Mtaalamu wa Tiba za Viungo, Sergio Perez Soto.
Akizungumza na mtandao rasmi wa klabu www.azamfc.co.tz
Kocha Mkuu Hernandez, alisema kuwa vyombo vingi vya habari katika eneo
la Tenerife wanaloishi vimekuwa vikiifuatilia timu hiyo na kuripoti
habari mbalimbali za Azam FC.
"Tuliporejea Hispania tulikutana na magazeti mbalimbali yakiielezea
Azam FC na kazi yetu tunayofanya hapa, makala nyingi zimekuwa zikielezea
kuwa kazi yetu itakuwa na umuhimu mkubwa kwa hapo baadaye ndani ya soka
la Afrika na klabu hii," alisema.
Alisema kuwa jambo jingine la umuhimu litakuwa pia ni kwa soka la
Hispania, kwani falsafa yetu itakuwa ikisambaa sehemu mbalimbali duniani
kutokana na makocha wa huko kuanza kusambaa duniani.
"La kufurahisha nililokutana nalo huko, ni Wahispania wengi kuanza
kuijua Azam FC na kuifutilia pia, hili ni jambo zuri kwa Azam FC,
duniani kuna nchi nyingi zinatamani kuwa na makocha kutoka Hispania,
lakini zinashindwa kuwapata na Azam FC imebahatika kwa ujio wetu hapa na
ndani muda mchache ujao itaanza kunufaika na ujio wetu hapa, ni suala
la muda tu," alisema.
Licha ya Azam FC kutopata matokeo mazuri kwenye baadhi ya mechi za
mzunguko wa kwanza wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara (VPL), mwanga
mzuri wa makocha hao umeanza kuonekana baada ya kuiongoza timu hiyo
kuandika rekodi mbalimbali ambazo huko nyuma zilishindikana kuwekwa.
Baada ya kusota miaka mitatu mfululizo bila kutwaa ubingwa na Ngao
Jamii, hatimaye mwaka huu Azam FC chini ya makocha hao imeweza kuandika
rekodi ya kubeba taji hilo kwa kuichapa Yanga kwa mikwaju ya penalti 4-1
kufuatia sare ya 2-2 ndani ya dakika 90 za mchezo huo.
Ikiwa ina rekodi mbaya huko nyuma ya kutoweza kuichapa Tanzania
Prisons nyumbani kwao ndani ya Uwanja Sokoine (Mbeya), msimu huu imeweza
kuichapa kwa mara ya kwanza (1-0) tokea ipande daraja mwaka 2008 na
kuwa timu pekee iliyozoa pointi zote sita ndani ya dimba hilo msimu huu
kufuatia kuichapa pia Mbeya City mabao 2-1.
Azam FC inayodhaminiwa na kinywaji safi cha Azam Cola kinachosisimua
mwili na kuburudisha koo pamoja na Benki bora kabisa nchini kwa usalama
wa fedha zako ya NMB, pia imeweza kuvuna jumla ya pointi tisa kati ya 12
kwenye mechi za ugenini za Kanda ya Ziwa.
Kati ya pointi hizo tisa, tatu ilivuna kwa kuibutua Toto African bao
1-0 ndani ya Uwanja wa CCM Kirumba (Mwanza) na kuandika rekodi ya
kushinda kwa mara ya kwanza ndani ya dimba hilo dhidi ya Wakishamapanda
hao, mechi nyingine za huko ikiichakaza Kagera Sugar 3-2 na Mwadui (4-1)
huku ikifungwa na Mbao (2-1).
Hadi inamaliza raundi ya kwanza ya ligi, Azam FC imefanikiwa kumaliza
katika nafasi ya tatu ikiwa na pointi 25 ikizidiwa 10 na kinara Simba
aliyejikusanyia 35 na Yanga ikiwa nafasi ya pili kwa pointi zake 33,
ambapo itaanza raundi ya pili kwa kumenyana na African Lyon Desemba 18
mwaka huu kwenye Uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam
No comments:
Post a Comment