KWA MAONI AU USHAURI E-mail: inocomm2014@gmail.com, PIGA SIMU: 0714555668

www.utt-pid.org


TEMBELEA: www.utt-pid.org

September 21, 2017

KAMATI YA BUNGE YAAHIRISHA KUMUHOJI KUBENEA


Kamati ya Bunge ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge, imeahirisha kumuhoji Mbunge wa Ubungo, Saed Kubenea kutokana na kufika mbele yake akiwa mgonjwa.

Kubenea amefika mbele ya kamati leo Jumatano saa nne asubuhi akiwa katika baiskeli ya wagonjwa (Wheel chair) chini ya ulinzi wa askari wa Jeshi la Polisi.

Mwenyekiti wa kamati hiyo, Kapteni mstaafu George Mkuchika amesema  walikutana kutokana na kupelekewa shauri na Spika la kumuita Kubenea akidaiwa kudharau mamlaka ya Spika kwa kauli alizozitoa katika kanisa moja jijini Dar es Salaam.

“Kamati ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge inakutana pale inapoletewa shauri na Spika, tumeletwa mashauri ya Kubenea ya kudharau mamlaka ya Spika kwa kauli ambazo amezitoa katika kanisa huko Dar es Salaam,” amekaririwa Mkuchika katika taarifa iliyotolewa na Bunge.

Amesema utaratibu unamtaka mtu anayetakiwa kufika mbele ya kamati hiyo kupelekewa hati ya kuitwa na kwamba alishapelekewa.

Mkuchika amesema Kubenea amepelekwa akiwa katika baiskeli ya wagonjwa na kuiomba kamati impangie siku nyingine kwa hiyo wameridhia ombi lake.

“Kamati baada ya kumsikiliza Kubenea imeridhia ombi lake la kumpangia tarehe nyingine kwa kumpa muda wa kuangalia afya yake mpaka atakapopona,”
 amesema.

Mkuchika aliagiza Kubenea apelekwe katika Zahanati ya Bunge ili apewe huduma ya kwanza.

Awali, Kubenea baada ya kuhojiwa na kamati kama ataweza kuzungumza katika kikao hicho aliiomba kamati kumpangia siku nyingine kwa kuwa asingeweza kuzungumza kwa wakati huo kutokana na kuwa katika maumivu makali.

Septemba 12, Spika wa Bunge, Job Ndugai aliagiza mbunge huyo kufika mbele ya kamati hiyo kuhojiwa kuhusu tuhuma alizozitoa wakati wa ibada Septemba 10  kwamba Spika alisema uongo bungeni wakati akitangaza idadi ya risasi zilizopigwa kwenye gari la Mbunge wa Singida Mashariki,  Tundu  Lissu.

No comments:

Post a Comment