KWA MAONI AU USHAURI E-mail: inocomm2014@gmail.com, PIGA SIMU: 0714555668

www.utt-pid.org


TEMBELEA: www.utt-pid.org

April 2, 2015

LOWASSA,SLAA WAONGOZA URAIS

Lowassa
 Utafiti uliofanywa na Taasisi ya Positive Thinkers Tanzania (PTT), umeonyesha kuwa Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa, anaongoza kati ya wanaotajwa kugombea urais katika uchaguzi mkuu wa Oktoba mwaka huu.
 
Utafiti huo pia unamuweka Katibu Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Dk. Willibrod Slaa katika nafasi ya pili.
 
Matokeo ya utafiti huo yamewapa nafasi za juu wanasiasa hao baada ya utafiti wa Shirika lisilo lwa kiserikali la Twaweza mwaka jana kumpa Lowassa nafasi ya kwanza na Dk. Slaa nafasi ya tatu.
 
Utafiti wa PTT yenye makao makuu jijini Dar es Salaam, matokeo yake yaliyotangazwa jana yanaonyesha kuwa Lowassa alipata kura 752 kati ya 3,298 zilizopigwa.
 
Dk. Slaa alipata kura 644 na Naibu wa Fedha, Mwigulu Nchemba 350.
 
Akitangaza ripoti ya utafiti huo jijini Dar es Salaam, Rais wa Taasisi hiyo, Tibatizibwa Gulayi, alisema ulifanywa katika mikoa 13 kwa kuwauliza wananchi kwa njia ya madodoso kisha taarifa zake kuingizwa katika mfumo wa Elektroniki unaojulikana kama Fast web application system (FWAS).
 
Alisema kuwa utafiti huo ulianza Februari, mwaka huu na kumalizika mwanzoni mwa Machi, mwaka huu na ulihusisha majina wanasiasa 15 wanaotajwa kuwania nafasi hiyo ya juu ya uongozi nchini.
 
Gulayi alisema wanasiasa wengine waliotajwa na kura zao kwenye mabano ni Mwenyekiti wa Chama cha Wananchi (CUF), Prof. Ibrahim Lipumba (294); Waziri wa Ujenzi, Dk. John Magufuli (227); Kiongozi Mkuu wa ACT – Tanzania,  Zitto Kabwe (224); Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe (197); Waziri  Mkuu, Mizengo Pinda (107) na Waziri wa Uchukuzi, Samuel Sitta (72).
 
Wengine ni Naibu waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, January Makamba (54); Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Kazi Maalum), Profesa Mark Mwandosya (40); Mwenyekiti wa NCCR-Mageuzi, James Mbatia (34) na Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa,  Dk. Hussein Mwinyi (31).
 
Waliofuatia ni Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika, Stephen Wasira (16) na Waziri Mkuu Mstaafu, Frederick Sumaye (10).
 
Watu ambao walisema hawana mgombea walikuwa 79 wakati waliosema mgombea yeyote atakayegombea ni sawa walikuwa 167.
 
CHANZO ;NIPASHE

No comments:

Post a Comment