Mwenyekiti wa CUF, Profesa Ibrahim Lipumba amefikishwa katika
Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu akikabiliwa na shtaka la kushawishi
wafuasi wake kutenda kosa la jinai.
Wakimsomea shtaka linalomkabili, mawakili wa
Serikali Joseph Maugo na Hellen Moshi walidai jana kuwa kati ya Januari
22 na 27 katika maeneo mbalimbali ya Dar es Salaam aliwashawishi wafuasi
wake kutenda kosa hilo kinyume cha sheria.
Baada ya kusomewa, Profesa Lipumba ambaye
anatetewa na mawakili; Mohammed Tibanyendera, Peter Kibatala, Hashimu
Mziray, Fred Kiwelu na John Malya alikana shtaka hilo na kudai kuwa ni
la uongo.
Upande wa mashtaka uliieleza Mahakama kuwa upelelezi wa kesi haujakamilika na kuiomba ipange tarehe nyingine.
Mawakili hao wa Profesa Lipumba waliiomba Mahakama
impatie mteja wao masharti ya dhamana yenye nafuu. Hakimu Mfawidhi,
Isaya Arufani alimtaka Profesa Lipumba kuwa na wadhamini wawili
wanaoaminika kila mmoja akiwa na barua na kitambulisho kila mmoja
kusaini hati ya dhamana ya maneno yenye thamani ya Sh2 milioni.
Profesa Lipumba alikamilisha masharti hayo na kuachiwa huru saa 9:42 alasiri. MWANANCHI
No comments:
Post a Comment