KWA MAONI AU USHAURI E-mail: inocomm2014@gmail.com, PIGA SIMU: 0714555668

www.utt-pid.org


TEMBELEA: www.utt-pid.org

January 27, 2015

MAAZIMIO YA ESCROW KUTIKISA BUNGE

Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania linaanza mkutano wake wa 18 leo, ambao pamoja na mambo mengine, wabunge wanatarajia kuhoji utekelezaji wa serikali wa maazimio nane ya Bunge kuhusu kashfa ya kampuni ya IPTL ya uchotwaji wa zaidi ya Sh. bilioni 300 kifisadi katika akaunti ya Tegeta Escrow, iliyokuwa Benki Kuu ya Tanzania (BoT).
 Maazimio hayo yaliyopitishwa na Bunge Zima, Novemba 29, mwaka jana, yalifuatia taarifa maalumu iliyowasilishwa bungeni na Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) kuhusu ukaguzi maalumu wa malipo yaliyofanyika katika akaunti hiyo.
 
Ukaguzi huo ulifanywa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) pamoja na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru).
 Taarifa hiyo ya PAC, iliyowasilishwa na Mwenyekiti wake, Zitto Kabwe, bungeni, Novemba 26, mwaka jana, ilieleza kuwa mmiliki wa kampuni ya Pan African Power Solutions Ltd (PAP), Harbinder Singh Sethi, mmiliki wa kampuni ya VIP Engineering & Marketing (VIP), James Rugemalira, walihusika kwa namna moja au nyingine katika kufanikisha kufanyika miamala haramu ya fedha katika akaunti hiyo kwenda kwa kampuni hizo.
 
Wengine waliotajwa na taarifa hiyo ya PAC kuhusika katika kashfa hiyo, ni Katibu Mkuu Wizara ya Nishati na Madini aliyesimamishwa kazi, Eliakim Maswi na aliyekuwa Waziri wa Nishati na Madini, Prof. Sospeter Muhongo aliyetajwa na PAC kuwa dalali kati ya Rugemalira na Sethi kufanikisha uchotwaji wa fedha hizo.
 Wamo pia aliyekuwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG), Jaji Frederick Werema na waliokuwa wajumbe wa Bodi ya Wakurugenzi wa Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco).
Hivyo, Bunge likaazimia kuwa Jeshi la Polisi na vyombo vingine husika vya ulinzi na usalama viwachukulie hatua stahiki za kisheria kwa mujibu wa sheria za nchi watu wote waliotajwa na taarifa hiyo ya PAC kuhusika na vitendo vyote vya kijinai kuhusiana na miamala ya akaunti hiyo na wengine watakaogundulika kuhusika katika vitendo hivyo.
 Kwa mujibu wa taarifa hiyo ya PAC, vitendo vilivyofanywa na watu hao vinaashiria makosa mbalimbali ya jinai, kama vile uzembe, wizi, ubadhirifu, kutakatisha fedha haramu, matumizi mabaya ya madaraka, rushwa na kupokea mali ya wizi.NIPASHE

No comments:

Post a Comment