KWA MAONI AU USHAURI E-mail: inocomm2014@gmail.com, PIGA SIMU: 0714555668

www.utt-pid.org


TEMBELEA: www.utt-pid.org

February 16, 2015

OPERESHENI KALI YAENDELEA TANGA



 Kikosi cha makomandoo cha JWTZ.

KUTOKANA na wahalifu waliopambana juzi na polisi na Jeshi la Wananchi (JWTZ) kutokamatwa, hali ya wasiwasi imeendelea miongoni mwa wakazi wa mjini hapa.
Sasa wananchi hao wameiomba Polisi kutoa tamko, kuhusu kikundi kilichorushiana risasi na askari Polisi na kusababisha kifo cha mwanajeshi mmoja.
Aidha, wananchi hao wameitaka Polisi kutoa ufafanuzi kuhusu mwendelezo wa matukio mengi ya uhalifu wa kutumia silaha, ambayo bado hayajapatiwa ufumbuzi, ikiwemo kutokamatwa kwa watuhumiwa wa matukio hayo.
Hata hivyo, Msemaji wa Polisi, Advera, alisema Jeshi lake halina taarifa zaidi ya iliyotolewa juzi na Mkuu wa Opersheni wa jeshi hilo, Kamishna Paul Chagonja.
Habari za kipolisi zinasema kwamba bado wanaendelea kusaka wahalifu hao huku baadhi ya vikosi vya ulinzi na usalama, vimeongezwa kwa ajili ya kupambana na wahalifu hao. Juzi Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) na Polisi walipambana na kundi la wahalifu katika maeneo ya mapango ya Amboni na kusababisha wanajeshi wanne na polisi wawili kujeruhiwa.
Hata hivyo, kuna habari kuwa majeruhi mmoja ambaye ni mwanajeshi alifariki baadaye akiwa hospitalini. Habari zingine zinasema kwamba majeruhi wengine ambao ni polisi wanne na mwanajeshi mmoja, wanaendelea vizuri.
Kuhusu mwanajeshi aliyekufa, polisi wamegoma kuzungumzia suala hilo, lakini habari zinasema aliyekufa ni mwanajeshi mwenye cheo cha sajenti. Wananchi wametoa kauli hizo kwa nyakati tofauti jana, walipozungumzia tukio la juzi, lililosababisha mapigano ya kurushiana risasi baina ya askari na wahalifu, wanaodaiwa kuficha silaha katika eneo la Mapango ya Amboni, nje kidogo ya mji wa Tanga.
Walisema mpaka sasa bado hawajaridhishwa na mwenendo wa utendaji wa Jeshi la Polisi mkoani hapa, pamoja na taarifa hafifu wanazotoa, kuhusu namna walivyoshughulikia tukio hilo la juzi kwenye mapango hayo ya Amboni.
Ibrahim Mshote, mkazi wa Ngamiani Kati, alisema mbali na tukio la juzi, yapo matukio mengine yakiwamo yaliyosababisha mauaji kwa raia, ambao walivamiwa na kuporwa mali na watuhumiwa kushindwa kupatikana. Alisema hakuna taarifa za mwendelezo wa kushughulikiwa kwa matukio hayo.
“Kwa mfano kuna wananchi walilipuliwa na bomu la kutupwa kwa mkono wakati wakitazama mpira kwenye kibanda cha video hapo Amboni… pia yupo mfanyabiashara wa eneo la Mkumbara wilayani Korogwe ambaye hivi karibuni alivamiwa na kuuawa kwa risasi kabla ya kuporwa mali, pia tukio la utekaji wa gari eneo la Michungwani wilayani Handeni baada ya kuwekewa magogo barabarani”, alisema.
Aliongeza “Katika matukio kama hayo, tunaambiwa tu wahalifu hawakupatikana, upelelezi unaendelea, lakini ni zaidi ya wiki mbili sasa hakuna taarifa zozote zinazoonesha juhudi za mwendelezo wa kudhibiti wahalifu kama hao, badala yake matukio yameendelea kuongezeka”.
Miriam Jonas, mkazi wa Barabara ya Tano jijini Tanga, alisema kitendo cha askari kunyang’anywa silaha mbili za SMG zenye risasi 60 kwenye kibanda cha chipsi ni fedheha kwa kuwa vitendo hivyo vilishasahaulika mkoani hapa.
“Tulitarajia wahusika wangekamatwa ndani ya muda mfupi, lakini wapi, Polisi hapa Tanga imeshindwa kabisa kutoa taarifa kuhusu tukio hilo hadi Kamishna Chagonja alipokuja na kuzungumzia tukio la juzi”, alisema.
Aidha, Mrisho Mashaka mkazi wa Kwaminchi alisema licha ya Chagonja kuwataka wakazi wa jiji la Tanga kutulia, kwakuwa hali ya usalama imeimarishwa, bado baadhi ya wananchi wanayo shaka na hofu kubwa kuhusu tamko hilo.HABARI LEO

1 comment:

  1. Watu mlio nje ya Tanga ndo mna hofu kubwa zaidi kuliko tuliomo huku. Watu tunaendelea na shughuli zetu kama kawaida.

    ReplyDelete