KWA MAONI AU USHAURI E-mail: inocomm2014@gmail.com, PIGA SIMU: 0714555668

www.utt-pid.org


TEMBELEA: www.utt-pid.org

June 18, 2015

BANDARI YA TANGA KUTUMIKA KUINGIZA MAFUTA.

Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji nchini (Ewura), Felix Ngamlagosi                                                                                                       Serikali itaanza kuitumia  Bandari ya Tanga kuingiza mafuta ifikapo Julai Mosi, mwaka huu, kwa lengo la kupunguza msongamano katika bandari ya Dar es Salaam.
 
Sababu nyingine ni kuinua uchumi wa mkoa wa Tanga pamoja na uharakishaji wa usafirishaji.
 
Aidha, waingizaji wa mafuta watakaotumia bandari hiyo watatumia gharama ndogo tofauti na kutumia bandari ya Dar es Salaam huku fedha zitakazopatikana zikiingia kwenye mfuko wa kuboresha bandari ya Tanga.  
 
Hayo yalisemwa jana jijini Dar es Salaam na Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji nchini (Ewura), Felix Ngamlagosi (pichani), katika mkutano na wadau wa mafuta ambao uliokuwa unajadili namna ya upangaji bei ya nishati hiyo kupitia bandari ya Tanga.
 
Alisema mwaka 2012 kulikuwa na mfumo wa uagizaji mafuta kwa pamoja ambao kwa kiasi kikubwa ulisaidia kupunguza gharama za uingizaji mafuta nchini na ukusanyaji kodi, akisisitiza kuwa imefikia wakati wa kutumia bandari hiyo kwani meli nyingi zinashusha mafuta bandari ya Dar es Salaam.  
 
“Serikali imeamua kufungua bandari ya Tanga ili kupunguza msongamano katika bandari ya Dar es Salaam pamoja na ucheleweshaji wa kupakua shehena za mafuta bandarini kwani utakuta mafuta yanachelewa mwezi mzima hivyo kusababisha gharama,” alisema.
 
Aidha, alisema haipendezi waagizaji wa mafuta kutumia bandari moja kuingiza mafuta na kuwa ikiwa Taifa litatumia bandari zaidi ya moja itasaidia kuharakisha usafirishaji wa nishati hiyo katika maeneo mbalimbali ya nchi na kukuza uchumi.
 
Ngamlagosi alisema mfumo huo utasaidia nchi kushindana vyema kibiashara na bandari za Mombasa (Kenya), Beira (Msumbiji) na Afrika Kusini na kuliingizia Taifa kipato kupitia wafanyabiahara wa nje wanaotumia bandari ya Dar es Salaam.
 
Aliongeza kuwa mchakato wa ukusanyaji maoni ya wadau wa mafuta ulifunguliwa Mei 19, mwaka huu huku ukitarajiwa kufungwa Juni 19, 2015.
 
Mwenyekiti wa Baraza la Walaji (Ewura CC), Prof. Jamidu Katima. alisema kuwa kazi kubwa ya baraza hilo  ni kuwatetea watumiaji wa nishati hiyo.
 
“Tunaambiwa meli za mafuta zikishusha katika banadari ya Tanga zitapunguza gharama kwa watumiaji hivyo tunapaswa kuliona hilo likitendeka,” alisema.
 
Prof. Katima alisema kwamba ikiwa mafuta yatakuwa yakishushwa katika bandari hiyo kwa bei nafuu ni wazi kuwa gharama za mafuta kwa watumiaji wa mikoa ya jirani na mkoa husika zitakuwa chini.

No comments:

Post a Comment