KWA MAONI AU USHAURI E-mail: inocomm2014@gmail.com, PIGA SIMU: 0714555668

www.utt-pid.org


TEMBELEA: www.utt-pid.org

June 20, 2015

DK. MWELE MALECELA: MSIUZE KURA KWA KUANGALIA FEDHA.

Dk. Mwele Malecela,                                                                                                                                 
Mgombea urais anayeomba ridhaa ya kuteuliwa na Chama cha Mapinduzi (CCM), Dk. Mwele Malecela (pichani), amewataka Watanzania kutouza kura zao kwa kuangalia fedha za muda mfupi.
 
Ameonya kuwa kwa  kufanya hivyo, watasababisha nchi kupata viongozi ambao hawatawasaidia kutatua changamoto zao.
Dk. Mwele aliyasema hayo jana wakati anazungumza na wadhamini kwa lengo la kuwashukuru, baada ya kumdhamini katika mkoa wa Kusini Unguja, visiwani Zanzibar.
 
Dk. Mwele alisema kuwa Watanzania wakichagua viongozi kwa sababu ya kupewa fedha watashindwa kuwawajibisha au kuhoji juu ya utendaji wao wa kazi pale wanapokwenda kinyume cha maadili ya uongozi.
 
“Watanzania tuwe makini kipindi hiki cha uchaguzi, unapochagua viongozi kwa kupewa fedha ujue siku ukimuelezea matatizo yako atakwambia tulishamalizana tangu kabla ya uchaguzi nilishakupa chako,” alisema.
 
“Kiongozi wa namna hiyo anaona kuwa kipindi cha kampeni alipokuwa akitoa fedha alikuwa anawalipa kwa kipindi atakachokaa madarakani ili afanye mambo yake na hatutaweza kumuuliza chochote wakati  huo,” alisema Dk. Mwele.
 
Dk. Mwele alisema kuwa vipaumbele vyake vipo ndani ya ilani ya Chama na kwamba atavieleza akishateuliwa kupeperusha bendera.
 
Alisema: “Wagombea wengi wamekuwa wakitaja vipaumbele vyao sambamba na kaulimbiu ila mimi nasubiri ilani kwa sababu siwezi kuahidi vitu wakati sijajua kama vimo kwenye ilani nitawadanganya.” Pia Dk. Mwele alisisitiza kudumishwa Muungano kwani ndio unaolitambulisha Taifa na watu wake nje ya nchi.
 
Alisema kizazi kilichopo kimeukuta Muungano katika hali nzuri, hivyo hakuna sababu ya kuwarithisha watoto wetu Muungano mbovu utakaozaa chuki na uhasama baina yao.
 
“Mimi nimezaliwa ndani ya Muungano na nimekulia ndani ya Muungano sijui chochote tofauti na Muungano kwa hiyo sina sababu ya kukitafuta nisichokijua,” alieleza.
 
“Kutafuta muundo wa Muungano au mfumo wa nchi tofauti na uliopo ambao tumeachiwa na waasisi wetu ni kutafuta tusichokijua, naomba Watanzania wenzangu tuudumishe Muungano, maana ndio umoja wetu na amani yetu,” alifafanua.
 
Akiwa kisiwani Pemba, Dk. Mwele aliwataka wana-CCM  wa Mkoa wa Kusini wilaya ya Chake Chake kuhakikisha CCM inakuwa imara katika maeneo hayo kutokana na kisiwa hicho kuwa ni ngome ya Chama cha Wananchi (CUF). 
CHANZO: NIPASHE

No comments:

Post a Comment