KWA MAONI AU USHAURI E-mail: inocomm2014@gmail.com, PIGA SIMU: 0714555668

www.utt-pid.org


TEMBELEA: www.utt-pid.org

June 17, 2015

KIKWETE ANA MGOMBEA?

Rais Jakaya Kikwete.                                                                                                                                 
Wakati msururu wa wanachama wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) wanaotafuta ridhaa ya chama kuteuliwa kuwania urais ukifikia watu 35, Rais Jakaya Kikwete, amekana kuwa na mgombea wake na badala yake ana kura moja ya kumchagua amtakaye.
 
Akizungumza na Waziri Mdogo wa Mambo ya Nje wa Marekani anayeongoza Kitengo cha Masuala ya Afrika Linda Thomas-Greenfield, mjini Johannesburg mwishoni mwa wiki iliyopita, Rais Kikwete alisema hana mgombea ana mpendelea kwa sababu wote ni wa kwake na wa chama chake.
 
Kwa mujibu wa taarifa kwa vyombo vya habari iliyotolewa na Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais, pia ilimnukuu Kikwete akisema kuwa hana tatizo na kujitokeza kwa wagombea wengi wa nafasi ya urais zamu hii kupitia CCM, kwa sababu hawezi kuwazuia kwa kuwa ni haki yao. Hata hivyo, alisema kuwa wingi wa wagombea zamu hii ni jambo zuri na ni ushahidi wa kiasi cha uhuru ambao umejengeka katika chama hicho na uthibitisho kuwa uongozi wa Tanzania katika miaka 10 iliyopita umekuwa wa mafanikio.
 
Rais Kikwete na Linda walikuwa wanahudhuria Mkutano wa 25 wa Kawaida wa Nchi Wanachama wa Umoja wa Afrika kwenye Kituo cha Mikutano cha Sandton Covention Centre, Johannesburg, Afrika Kusini uliomalizika juzi.
 
Hadi jana CCM ilikuwa na wanachama 35 ambao wamejitokeza kutafuta ridhaa ya chama hicho kuteuliwa kuwania urais katika uchaguzi mkuu wa Oktoba 25, mwaka huu.
 
Waliokwisha kujitokeza hadi jana ni Makamu wa Rais, Dk. Muhamed Gharib Bilal, Waziri Mkuu, Mizengo Pinda; Waziri wa Uchukuzi, Samuel Sitta; Waziri wa Ujenzi, Dk. John Magufuli; Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika, Stephen Wasira na Waziri wa Uvuvi na Maendeleo ya Mifugo, Dk. Titus Kamani.
 
Wengine ni Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Kazi Maalum, Prof. Mwandosya; Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mathias Chikawe; Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe na Waziri wa Sheria na Katiba, Dk. Asha-Rose Migiro.
 
Pia wamo Waziri wa Maliasili na Utalii, Lazaro Nyalandu; Naibu Waziri wa Fedha, Mwigulu Nchemba na Naibu Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, January Makamba.
 
Mbali na mawaziri hao, wapo mawaziri wakuu wa zamani, Edward Lowassa na Frederick Sumaye.
 
Makada wengine ni Mbunge wa Nzega, Dk. Hamis Kigwangalla; Mbunge wa Sengerema, William Ngeleja; Mbunge wa Kuteuliwa, Profesa Sospeter Muhongo; Maliki Marupu; Joseph Chagama; Makongoro Nyerere; Mwale Malecela; Monica Mbega; Balozi Ali Karume, Balozi Amina Salum Ali na Balozi Augustine Mahiga.
 
Hadi sasa walikwisha kurejesha fomu ni Sitta na Dk. Bilal, wengine wanaendelea kusaka wadhamini mikoani.
 
Kamati Kuu (CC) ya Chama hicho itakutana Julai 12, mwaka huu kuwachuja wagombea na kubaki na majina matano ya kupeleka mbele ya mkutano wa Halmashauri   Kuu   ya   Taifa  (NEC).
 
Kazi ya kuchuja ni nzito kwani miongoni mwa wajumbe wa CC kuna watia nia kama Dk. Bilal; Pinda Wasira na Dk. Migiro.

No comments:

Post a Comment