KWA MAONI AU USHAURI E-mail: inocomm2014@gmail.com, PIGA SIMU: 0714555668

www.utt-pid.org


TEMBELEA: www.utt-pid.org

June 16, 2015

MIGIRO ACHUKUA FOMU, ASEMA HAKUBEBWA UN.

Waziri wa Katiba na Sheria, Dk. Asha-Rose  Migiro                                                        Waziri wa Katiba na Sheria, Dk. Asha-Rose Migiro, jana alichukua fomu ya kugombea urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), akisema hakuupata wadhifa wa Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa (UN), kwa kupewa kama zawadi au urafiki, isipokuwa alikidhi vigezo vya kiongozi aliyetakiwa kutoka Bara la Afrika.
 
“Ilikuwa ni zamu ya Afrika na ilikuwa lazima atoke Tanzania, bahati ikawa kwa Asha-Rose, lakini si kama inavyofikiriwa kwamba kuna urafiki, zawadi au hisani ilitolewa ndio nikaipata. Uongozi katika UN unapitia mchujo, unachunguzwa kwa muda mrefu na wala hakuna kupewa kazi kwa ujamaa,” alisema Dk. Migiro.
 
Akizungumza na waandishi wa habari katika Makao Makuu ya CCM Mjini Dodoma jana alasiri  baada ya kuchukua fomu, Dk. Migiro alisema alichaguliwa kuwa Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa kutokana na uwezo wake pamoja na sifa alizonazo; ndio maana Katibu Mkuu wa Umoja huo, Ban Ki-Moon, alimkubali pasipo shaka.
 
Waziri Migiro alisema uamuzi alioufanya wa kutangaza nia ya kugombea urais, unatokana na CCM kupanua wigo wa demokrasia kwa kuwawezesha wanachama wengi zaidi kujitokeza katika mchakato wa kumtafuta kiongozi muhimu wa Taifa.
 
“Mazingira mazuri na mafanikio yaliyojengwa na kufikiwa na CCM katika awamu zote nne, yamenisukuma mimi kuwa mwanamke wa tatu kutangaza nia ya kugombea nafasi ya urais, kati ya makada wengine 32 waliotangulia; nafarijika sana na wigo wa demokrasia uliopo,” alisisitiza.
 
Kuhusu vipaumbele vyake akiteuliwa kuwa mgombea urais, Dk. Migiro alisema: “Nasubiri ilani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) inayoandaliwa ili niitumie kama nyenzo kuu ambayo itakuwa imetaja maeneo yote muhimu.”
 
Hata hivyo, Waziri Migiro alisema mafanikio yaliyofikiwa na serikali ya awamu ya nne, yamechochea ukuaji wa uchumi na uboreshaji wa huduma za afya na hivyo kuongeza umri wa kuishi kutoka miaka 45 hadi 60.
 
Dk. Migiro aliondoka nchini, Januari 5, mwaka 2007 akiwa Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, baada ya kuteuliwa kuwa Naibu Katibu Mkuu wa UN na kuhudumu hadi alipomaliza muda wake, mwezi Januari mwaka 2014.
 
Baada ya kurejea nchini, aliteuliwa kuwa Katibu wa Halmashauri Kuu ya Taifa ya Chama Cha Mapinduzi (NEC), Idara ya Siasa na Uhusiano wa Kimataifa.
                                                       

No comments:

Post a Comment