KWA MAONI AU USHAURI E-mail: inocomm2014@gmail.com, PIGA SIMU: 0714555668

www.utt-pid.org


TEMBELEA: www.utt-pid.org

September 22, 2015

BILAL AWATAKA WAUMINI KULIOMBEA TAIFA

WAUMINI wa dini mbalimbali nchini wamehimizwa kuliombea taifa katika wakati huu wa kuelekea uchaguzi mkuu ili shughuli hiyo iweze kumalizika kwa amani na utulivu. Makamu wa Rais, Dk Mohamed Gharib Bilal alihimiza hayo kwenye ibada maalumu ya kuwekwa wakfu Askofu wa Kanisa la Moravian Jimbo la Kusini, mchungaji Kenan Panja iliyofanyika mjini Tukuyu wilayani Rungwe.


Dk Bilal alisema kwa kiasi kikubwa sala na dua za viongozi wa madhehebu yote ya dini nchini zimesaidia kuleta baraka na kudumisha utulivu na mshikamano nchini. Alisema viongozi wa serikali wamejipanga vilivyo kuhakikisha zoezi la uchaguzi linafanyika kwa amani na utulivu na kubainisha kuwa serikali itasimamia na kuhakikisha uchaguzi unakuwa huru na wa haki.


“Nawaomba viongozi wa dini zote nchini kuhamasisha waumini wao kujitokeza kwa wingi siku ya kupiga kura ili kutekeleza haki yao ya msingi kikatiba, kwa kuchagua viongozi bora watakaoongoza taifa letu katika kipindi cha miaka mitano ijayo.


“Amani ni sharti la kwanza katika maendeleo ya wanadamu. Vitabu vya dini zote duniani vinafundisha umuhimu wa amani kwa wanadamu. Yesu Kristo alipofufuka na kukutana na wanafunzi wake kwa mara ya kwanza neno lake la kwanza aliwaambia Amani iwe kwenu.


Hakutaja jambo lingile lolote. Alitamka hilo kwa kutambua kwamba ndani ya Amani kuna kila kitu,” alisema. Dk Bilal alisema palipo na amani pana maendeleo, ustawi, uchumi mzuri, furaha na upendo hivyo kama taifa ni wajibu wa kila mmoja kudumisha amani, umoja na mshikamano vilivyojengwa kwa muda mrefu chini ya misingi imara iliyowekwa na waasisi wa taifa, Mwalimu Julius Nyerere na Abeid Amaan Karume.


Alihakikisha kuwa viongozi waliopewa dhamana watahakikisha Tanzania inaendelea kuwa kisiwa cha amani, umoja na mshikamano akisema hata maandiko matakatifu yanaelekeza kuwa Atukuzwe Mungu juu mbinguni na duniani iwe amani kwa watu aliowaridhia.


Aliwasihi waumini wa dini zote kukataa mitego yote inayoweza kuwanasa na kusambaratisha umoja wa taifa, hususani katika kipindi hiki cha uchaguzi mkuu. Kwa upande wake Askofu i Panja alisema changamoto za kimaisha zinazowakabili waumini ni mambo yanayohitaji mchango wa viongozi wa dini kushirikiana na watawala wa taifa kutafuta ufumbuzi kupitia umoja na mshikamano.

No comments:

Post a Comment