KWA MAONI AU USHAURI E-mail: inocomm2014@gmail.com, PIGA SIMU: 0714555668

www.utt-pid.org


TEMBELEA: www.utt-pid.org

October 3, 2016

SITA WACHAGULIWA UDHAMINI WA MASOMO VYUO VIKUU 2016/17




Wanafunzi sita waliofanya vizuri sana katika mitihani wa taifa ya Kidato cha Sita ya mwaka 2016 na shahada ya kwanza wameshinda udhamini wa elimu ya chuo kikuu kwa mwaka wa 2016/17 kupitia Mfuko wa Udhamini wa Elimu wa Kumbukumbuku ya Mwalimu Julius Nyerere unaosimamiwa na Benki Kuu ya Tanzania (BoT).

Mwenyekiti wa Kamati ya Udhamini ya Mfuko huo na Naibu Gavana wa BoT, Dkt. Natu Mwamba alisema katika taarifa yake kwamba kati ya hao sita, wanne ni wanafunzi wa kike na wawili wa kiume, ambapo kati yao wanne watadhaminiwa kusomea shahada ya kwanza na wawili shahada ya uzamili katika masomo ya science na hisabati.

Waliochaguliwa kudhaminiwa shahada ya kwanza ni miongoni mwa wanafunzi bora 10 katika matokeo ya Mtihani wa Taifa wa Kidato cha Sita kwa mwaka 2016, na watakaodhaminiwa shahada ya uzamili walipata ufaulu juu wa Daraja la Kwanza katika mitihani yao ya shahada ya kwanza.

Dkt. Mwamba aliwataja waliochaguliwa kozi za shahada ya kwanza watakaosoma Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kuwa ni Bi. Magreth Deusdedith Kakoko (Sayansi Uhandisi Ujenzi) Bi. Bertha Peter Nguyamu (Sayansi Uhandisi wa Mafuta na Bw. Japhet Swema Lawrence (Biashara – Uhasibu). Bi. Juliana Elias Mwalupindi (Uhasibu, Sekta ya Biashara) atasoma katika Chuo Kikuu cha Mzumbe. Aidha, Bw. Shega Mayila na Bi. Elizabeth Elisey Mrema wanadhaminiwa kusoma shahada ya uzamili (Sayansi – Hisabati) katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.

Mfuko wa Udhamini wa Elimu wa Kumbukumbu ya Mwalimu Julius Nyerere ulianzishwa na BoT mnamo tarehe 12 Oktoba, 2009 kama njia ya kuenzi mafanikio makubwa ya Rais wa kwanza wa Tanzania, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere.

Lengo kuu la Mfuko huu ni kuongeza hamasa na ufaulu kwa wanafunzi wa kike hapa nchini katika masomo ya Hisabati na Sayansi. Mfuko umejikita kutoa udhamini kwa wasichana wanaofanya vizuri katika mitihani ya taifa ya Kidato cha Sita kuweza kusoma shahada ya kwanza kozi za hisabati na sayansi katika vyuo vikuu hapa nchini.

Sehemu ya udhamini huo hutumika pia kwa wanafunzi wa kike na wa kiume waliofanya vizuri katika mitihani ya Kidato cha Sita kusomea shahada za uchumi, teknolojia ya habari na mawasiliano (TEHAMA), uhasibu na fedha na wanafunzi wote wa kike na kiume kusomea shahada ya uzamili katika masomo hayo.

Mfuko ulianza kutoa udhamini 2013/14. Hadi hivi sasa jumla ya Watanzania 22 wamepata udhamini huo; kati yao 16 ni wanawake na 6 ni wanaume. Baadhi yao wamekwishamaliza kozi zao na kupata ufaulu wa juu na wengine wanaendelea na masomo yao katika fani za Uhandisi-Mafuta na Gesi, Sayansi ya Mafuta na Jiolojia, Udaktari, Ufamasia, Usanifu Majengo, Sayansi (Kemia), Sayansi - Uchambuzi wa Masuala ya Bima (actuarial sciences), Uhasibu, Fedha, Uchumi na Takwimu, TEHAMA na Uongozi.

Udhamini unaotolewa chini ya Mfuko huu unahusu gharama zote za masomo zinazolipwa moja kwa moja kwa vyuo vikuu husika na zile ambazo zinalipwa kwa wanafunzi kulingana na mahitaji ya masomo yao. Aidha, kila mwanafunzi hupewa kompyuta mpakato (laptop) kwa ajili ya kumsaidia katika masomo yake.

Aidha, tangu mwaka 1994 BoT imekuwa ikitoa udhamini ujulikanao kama Gilman Rutihinda Scholarships kwa wanafunzi waliofanya vizuri katika shahada zao za kwanza kusoma shahada ya uzamili. Hadi Februari mwaka huu, jumla ya wanafunzi bora 31 wamedhaminiwa kusoma shahada ya uzamili katika masuala ya uchumi, fedha na biashara ya kimataifa katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na Chuo Cha Usimamizi wa Fedha (IFM).

Imetolewa na Idara ya Uhusiano wa Umma na Itifaki
03-10-2016



No comments:

Post a Comment